Friday, November 11, 2016


Rais Magufuli aongoza mamia ya Watanzania kuaga mwili wa Samuel Sitta



Mwili wa aliyekuwa spika wa bunge la Tanzania, Samuel Sitta umeagwa katika viwanja vya Karimjee na mamia ya watanzania wakiongozwa na Rais wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli na Makamu wa Rais mama Samia Suluhu.

 Wengine ni Rais mstaafu wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete, Dk. Gharib Bilal.Baada ya kuagwa Dar, mwili wake utapelekewa Dodoma kwa ajili ya wabunge kutoa saamu za mwisho kisha kupelekwa Urambo, Tabora.

Friday, November 11, 2016


Agizo la Serikali kwa wanafunzi waliohitimu kidato cha sita mwezi Mei mwaka huu Ambao Hawakujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT)



Serikali amewaagiza wote waliohitimu kidato cha sita Mei mwaka huu na ambao hawajajiunga na vyuo vya elimu ya juu, wakaripoti katika kambi za Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Desemba Mosi, mwaka huu.

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi ametoa agizo hilo mjini Dodoma alipozungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Habari wa Bunge.

Dk Mwinyi alisema Mei na Juni mwaka huu, JKT iliwafanyia usaili vijana wa kujiunga na JKT kwa kujitolea. Alisema usaili huo ulifanyika kwa kushirikiana na kamati za ulinzi za wilaya na mikoa.

“Wizara ya Ulinzi na JKT inapenda kuwatangazia vijana wote waliosailiwa Juni mwaka huu, kujiunga na JKT kwa kujitolea, waripoti kwenye kambi walizopangiwa ifikapo Desemba Mosi mwaka huu kwa nauli zao,” amesema Dk Mwinyi.

Dk Mwinyi amesema mafunzo hayo ni ya miezi mitatu kwa mafunzo yenye utaratibu wa kawaida na miaka miwili kwa wa kujitolea.

Ili kufanikisha hilo, Wizara ilimuagiza Mkuu wa JKT kufufua kambi ya Makuyuni JKT iwe miongoni mwa kambi kuanzia Desemba mwaka huu.

Aliagiza kambi za Luwa na Milundikwa za mkoani Rukwa, zirejeshwe kwa shughuli za JKT za kilimo na ufugaji.

Dk Mwinyi alimuagiza Mkuu huyo wa JKT pia kambi ya Mpwapwa irejeshwe kwa ajili ya kuendesha mafunzo ya kilimo na ufugaji ndani ya JKT.

Friday, November 11, 2016


Mahakama Yampa Siku 7 Profesa Lipumba na Msajili wa Vyama Kujibu Hoja za CUF



Mahakama Kuu imewapa siku saba Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba na wenzake kujibu madai ya chama hicho.

Msajili, Lipumba na wenzake walipewa muda huo jana na Jaji Sekieti Kihiyo kutokana na kesi ya madai iliyofunguliwa na Bodi ya Wadhamini wa CUF mahakamani hapo.

Katika kesi hiyo namba 23 ya mwaka 2016, bodi ya wadhamini CUF inaiomba mahakama itoe amri ya kubatilisha barua ya Msajili inayomtambua Profesa Lipumba kuwa ndiye mwenyekiti wa chama hicho.

Pia, wanaiomba mahakama itoe amri ya kumzuia Msajili kufanya kazi nje ya mipaka yake ya kisheria katika utekelezaji wa majukumu yake na pia itoe amri ya kumzuia Msajili kuingilia masuala ya kiutawala ndani ya chama hicho.

Mbali na Msajili na Profesa Lipumba, wadaiwa wengine katika kesi hiyo ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) na wanachama wengine tisa waliosimamishwa uanachama wa chama hicho, akiwamo Naibu Katibu Mkuu Bara ambaye pia ni Mbunge wa Kaliua (Tabora), Magdalena Sakaya.

Kesi hiyo ilitajwa jana mahakamani hapo kwa mara ya kwanza tangu ilipofunguliwa Oktoba 19, mwaka huu na mahakama ikataka wadaiwa kuwasilisha majibu ya madai hayo ya CUF, Novemba 17, mwaka huu.

Pia, Mahakama ilielekeza upande wa Maalim Seif kuwasilisha majibu ya hoja za wadaiwa Novemba 23 na ikapanga kesi hiyo itajwe tena Novemba 24, kwa ajili ya kuendelea na hatua nyingine.

Wadai katika kesi hiyo wanawakilishwa na mawakili Juma Nassoro na Halfani Daim wakati Msajili na Mwanasheria Mkuu wa Serikali wanawakilishwa na Wakili wa Serikali Mkuu (PSA), Obadia Kameya na Lipumba na wenzake wakiwakilishwa na Mashaka Ngole.

Katika hati ya Kiapo kinachounga mkono maombi hayo, Maalim Seif anadai kuwa Msajili wa Vyama vya Siasa hana mamlaka ya kuingilia utendaji wa ndani wa Vyama vya Siasa.

Anadai kuwa Sheria ya Vyama vya Siasa na Katiba ya nchi haimpi mamlaka Msajili wa Vyama vya Siasa kuwa chombo cha rufaa wala kurejea mambo ya utawala ndani ya chama cha siasa.

Badala yake anadai mamlaka hayo yako kwa vyombo vya juu vya chama na Mahakama na kwamba jukumu la Msajili ni kusajili vyama na kuweka kumbukumbu za vyama hivyo.

CUF kimekuwa na mgogoro wa kiuongozi baada ya Profesa Lipumba kuandika barua ya kutengua uamuzi wake wa awali wa kujiuzulu ambao Msajili alikubaliana naye na alikiandikia barua chama kuendelea kumtambua mwenyekiti huyo. Hata hivyo, CUF ilimfukuza uanachama Lipumba.

Friday, November 11, 2016


Misiba Yasitisha Mkutano wa Bunge Mjini Dodoma Leo



Mkutano wa Tano  wa Bunge umeahirishwa kwa namna yake baada ya muhimili huo wa dola kupata misiba mikubwa miwili.

Misiba hiyo ni wa Spika Mstaafu, Samuel Sitta aliyefariki nchini Ujerumani na Mbunge wa Dimani(CCM) Hafidh Ally ambaye alifariki dunia usiku wa kuamkia leo (Ijumaa) katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Dodoma.

Mara baada ya kutangaza  kifo cha Hafidh Spika wa Bunge,  Job Ndugai alimtaka Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge, Ajira, Kazi, Vijana Jenista kutengua kanuni ili  kuwezesha mambo vote kufanyika.

Spika alimtaka Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Sheria  Ndogo Ndogo, Andrew Chenge kuhitimisha hoja yake ya taarifa ya Kamati iliyowasilishwa juzi bila kujadiliwa na wabunge ili  Serikali yaweze kufanyia kazi.

Baada ya kufanya hiyo, Spika ameahirisha bunge hadi saa  8.30 mchana kwa ajili ya kikao maalum cha Bunge.

Amesema mara  baada kikao maalum cha bunge kumuaga Sitta basi  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa atatoa hoja yake kuahirisha Bunge kwa  kifupi sana  tofauti na wakati mwingine.

Friday, November 11, 2016


LIVE: Fuatilia Hapa Zoezi la Kuuaga Mwili wa Samwel Sitta ambalo Linaongozwa na Rais Magufuli



Leo kuna shughuli ya kuaga mwili wa aliyekuwa Spika wa Bunge la Tisa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pia Spika wa Bunge Maalum la Katiba(BMK), Marehemu Samwel Sitta.

Rais Magufuli ataongoza waombolezaji kuuaga mwili wa Marehemu Sitta katika Viwanja vya Karimjee.

Friday, November 11, 2016


BOT Yasitisha Kuweka Dhahabu Kama Hazina Ya Rasilimali Za Kigeni





Benki Kuu ya Tanzania (BOT) imesitisha kuweka dhahabu kama hazina ya rasilimali za kigeni kwa sababu ya kuyumba kwa bei ya madini hayo katika soko la dunia na kusababisha uwezekano wa kupunguza thamani ya hazina ya rasilimali ya nchi.

Kauli hiyo imetolewa jana mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt Ashatu Kijaji alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Igunga Mhe. Dalaly Kafumu aliyehitaji kufahamu sababu za Serikali kukataa kutunza dhahabu safi katika Benki Kuu wakati Tanzania ni nchi mojawapo inayozalisha dhahabu safi.

Mhe. Kijaji alisema kuwa jukumu la msingi la Benki Kuu ni kuandaa na kutekeleza Sera ya Fedha inayolenga kuwa na utulivu wa bei kwa ajili ya ukuaji endelevu wa uchumi wa Taifa hivyo ili kufanikisha azma hiyo Benki Kuu inadhibiti ongezeko la ujazi wa fedha kwa kutumia nyenzo mbalimbali zikiwemo za kuuza dhamana na hati fungani za Serikali pamoja na kushiriki katika soko la jumla la fedha za kigeni kati ya mabenki.

“Katika kutekeleza jukumu lake la msingi, Benki Kuu hutunza hazina ya rasilimali za kigeni zinazotosha kuagiza bidhaa nje kwa kipindi kisichopungua miezi minne lakini kwa muda mrefu sasa Benki Kuu ya Tanzania haiweki dhahabu kama sehemu ya rasilimali hizo kutokana na kuyumba kwa bei ya dhahabu katika soko la dunia”, alisema Mhe. Kijaji.

Naibu Waziri huyo alitoa mfano wa kushuka kwa bei ya dhahabu katika soko la Dunia ambapo dhahabu ilishuka kutoka dola 1,745 za kimarekani katika mwezi Septemba 2012 hadi dola za kimarekani 1,068 kufikia mwezi Desemba 2015.

Mhe. Kijaji alifafanua kuwa hazina ya rasilimali za kigeni zinaweza kuwa dhahabu – fedha (monetary gold) au fedha za kigeni ambapo uamuzi kuhusu hazina itunzwe vipi unazingatia vigezo mbalimbali vikiwemo vile vya kudumisha thamani, wepesi wa kubadilisha pamoja na faida inayopatikana kwa kuwekeza hazina hiyo.

Aidha, Mhe. Kijazi alisema kuwa ununuzi na uuzaji wa madini ya dhahabu unahitaji ujuzi maalum ambapo kwa kuzingatia jukumu la msingi la Benki Kuu inaonyesha dhahiri kuwa Benki hiyo haijajijengea uwezo katika eneo la biashara ya madini hayo.

Friday, November 11, 2016


TANZIA: Mbunge Hafidh Ali Tahir Afariki Dunia Alfajiri ya Leo Akiwa Mjini Dodoma



Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzaia, Job Ndugai (Mb) anasikitika kuwatangazia kuwa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Dimani, Zanzibar, Hafidh Ali Tahir amefariki dunia leo saa 9 alfajiri katika Hospitali ya General mkoani Dodoma.

 Spika anaungana na Wabunge wote katika kuomboleza msiba huu.

Awali Marehemu pia alikuwa mwalimu wa soka kwenye timu ya Bunge Sports Club na mpaka usiku wa Novemba 10 alikuwa pamoja na Wabunge katika vikao  mpaka saa 2.45 usiku.

Friday, November 11, 2016


Picha 5: Mwili wa Spika Mstaafu Samwel Sitta Uliyopokelewa Airport Jijini Dar es Salaam



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan jana aliongoza viongozi na wananchi katika mapokezi ya Mwili wa Spika Mstaafu Samuel Sitta katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam ukitokea nchini Ujerumani alipofariki wakati anapatiwa matibabu.

Akizungumzia jinsi anavyomfahamu Samuel Sitta katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan alisema Taifa limeondokewa kiongozi mwadilifu,mzalendo, mchapakazi na mtetezi wa wanyonge hivyo taifa litaendelea kuumuenzi utendaji wake.

Viongozi mbalimbali waliojumuika na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan katika mapokezi ya mwili wa Spika Mstaafu Samweli Sitta kweye Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Julius Nyerere ni pamoja na Makamu wa Pili wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Seif Ali Iddi, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika, Kikanda na Kimataifa Dkt Augustine Mahiga na Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda.

Baada ya Mwili wa Spika Mstaafu Samuel Sitta kuwasili nchini jana mchana alipelekwa nyumbani kwake Masaki jijini Dar es Salaam ambapo leo  asubuhi viongozi na wananchi watatoa heshima zao ya mwisho za kuuaga mwili wa marehemu katika viwanja wa Karimjee jijini.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu  Hassan akimpokea mjane wa Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri Mwandamizi Mstafu Marehemu Samuel Sitta, Mama Margaret Sitta (kushoto) mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwaongoza viongozi mbali mbali wakati wa mapokezi ya mwili wa Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri Mwandamizi Mstafu Marehemu Samuel Sitta

 

 

 

Friday, November 11, 2016


Reli ya Standard Gauge kutoka Dar-Mwanza kuanza kujengwa Disemba, 6 mwaka huu



Hatua ya kwanza ya maandalizi ya ujenzi wa reli ya Standard Gauge imeshaanza ambapo awamu ya kwanza ya ujenzi huo kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza itaanza rasmi Disemba 6, 2016.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli Tanzania (RAHCO) Masanja Kadogosa amesema serikali imetenga trilioni 1 kwa ajili ya ujenzi huo.

“Ujenzi wa reli ya standard gauge umeshaanza lakini hatua iliyokuwepo haionekani, tenda zimeshaanza kutangazwa,” alisema  Kadogosa  wakati akiongea  na  waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam.

Alisema ujenzi huo utaanza kwa awamu na kwamba awamu ya kwanza inatarajiwa kuanzwa Disemba 6, 2016 wakati ya pili itaanza Februari 15, 2016.

“Ujenzi huo utachukua miaka mitatu kukamlika, ambapo utaleta manufaa kwa kizazi cha sasa na kijacho. Pia utarahisisha usafirishaji wa mizigo kutokana na kwamba litakuwa na mabehewa yenye kilomita 2 ambayo sawa na ukubwa wa maroli 300,” alisema.

Alisema wamiliki wa majengo yatakayo athiriwa na ujenzi huo watalipwa fidia.

“Hifadhi ya reli ina maana kwamba kila upande inaachwa mita 30, hivyo kama kuna nyumba zitakazokuwa nje ya mita hizo zitatakiwa kubolewa wamiliki watalipwa fidia,” alisema.

Aidha, Kadogosa alisema kuna miradi mingine midogo ya ujenzi na ukarabati itafanyika ikiwemo ya ujenzi wa reli mpya ya Dar es Salaam ambayo itatumiwa kwa ajili ya usafiri kwa wakazi wa jiji hilo.

“Kuna Mradi wa kujenga reli mpya katika jiji la Dar es Salaam na viunga vyake kwa ajili ya treni za abiria ili kupunguza msongamano wa abiria na magari. Mradi huu uko katika hatua ya upembuzi yakinifu na usanifu wa awali chini ya kampuni ya ushauri ya GIBB Engineering ya Afrika Kusini na kwamba inatarajiwa kukamilika Disemba 2016,” alisema.


 

Friday, November 11, 2016


Picha: Rais Magufuli Alivyoongoza wananchi wa Dar kuaga mwili wa Marehemu Joseph Mungai


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, jana tarehe 10 Novemba, 2016 aliwaongoza viongozi na wananchi wa Dar es Salaam kuuaga mwili wa Waziri na mbunge Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Joseph James Mungai katika ukumbi wa Karimjee Jijini Dar es Salaam.

Pamoja na Rais Magufuli Viongozi wengine waliofika kuuaga mwili wa Marehemu Mungai ni Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin William Mkapa, Makamu wa Rais Mstaafu,  Mohamed Gharib Bilal, Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba, Waziri Mkuu Mstaafu. Frederick Tluway Sumaye, Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi na Viongozi wengine mbalimbali wa Serikali na Siasa.

Joseph James Mungai alifariki dunia tarehe 08 Novemba, 2016 katika hospitali ya Taifa Muhimbili baada ya kuugua ghafla na mwili wake utasafirishwa leo Ijumaa kwenda Mafinga Mkoani Iringa kwa Mazishi
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na waombolezaji waliofika kuaga mwili wa Marehemu Joseph Muungai katika Ukumbi wa Karimjee jijini Dar es salaam Novemba 10,2016
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, Rais Mstaafu awamu ya tatu Benjamin Mkapa pamoja na waombolezaji  wengine walipofika kuaga mwili wa Marehemu Joseph Muungai katika Ukumbi wa Karimjee jijini Dar es salaam Novemba 10,2016

Reviewed by RICH VOICE on Novemba 11, 2016 Rating: 5

Hakuna maoni

Chapisho Lililoangaziwa

Thursday, September 15, 2016 Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Alhamisi Ya Septemba 15 ...