Samia aokoa milioni 33/- safari ya ATCL


KATIKA kuendelea kujenga dhana ya kubana matumizi ya fedha za serikali, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan amesafiri kwa ndege ya abiria ya Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) kutoka Dar es Salaam kwenda Mwanza na kuokoa zaidi ya Sh milioni 33.
Kabla ya kuanza safari hiyo jana kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam, Makamu wa Rais akizungumza na waandishi wa habari, alisema kwa kupanda ndege hiyo ameokoa fedha za serikali na kodi za wananchi.
Alisema ameona ashirikiane na Watanzania kuonesha uzalendo kwa kutumia huduma ambazo zinatolewa na serikali na kuwataka Watanzania wote kutumia ndege hizo.
“Ningepanda ndege ya kukodi ningetumia shilingi milioni 40 kwa safari hii, lakini nikaona hapana nikaamua mimi pamoja na msafara wangu tutumie ndege hii ya Shirika la Ndege Tanzania ambapo tumetumia Shilingi milioni 7.6 pekee,” alisema Makamu wa Rais aliyeambatana na watu 16 katika safari hiyo.
Makamu wa Rais ambaye alipanda ndege hiyo pamoja na abiria wengine wa kawaida, aliwataka viongozi wengine pia kufuata mfano huo kusafiri kwa kutumia ndege za shirika hilo.
Alisema ameona kwenye televisheni watu wakitoa maoni yao juu ya kampuni hiyo ya ndege kuwa ni nzuri kwa sasa na yeye akaamua kusafiri na ndege hiyo.
“Niliona kwenye televisheni watu wakitoa maoni mazuri tu juu ya shirika hili na mimi nikaona nitumie nafasi hiyo,” alifafanua Makamu wa Rais.
Hivi karibuni, serikali imenunua ndege mbili aina ya Bombardier Q400 na kuzikabidhiwa kwa ATCL na zimeanza kufanya kazi katika mikoa mbalimbali nchini huku zikiwa na gharama nafuu, lakini pia zikiwa na gharama nafuu ya uendeshaji.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa ambaye alikuwepo uwanjani akimsindikiza Makamu wa Rais, alisema Watanzania waelewe kwa sasa kampuni hiyo iko kwa ajili ya kufanya biashara.
Alimpongeza Makamu wa Rais kwa kuonesha ushirikiano mkubwa na pia uzalendo kwa kusafiri na ndege ya ATCL, kwani angeweza kutumia ndege nyingine yoyote.
“Leo hii kwa kutumia ndege ya Tanzania yeye pamoja na wasaidizi wake ni jambo jema sana alilolifanya na pia ni jambo la kizalendo tunampongeza sana, kwani angeweza kutumia ndege nyingine yoyote anayoitaka,” alisema Profesa Mbarawa.
Alisema ndege za ATCL gharama zake ni nafuu na pia huduma zao zimeboreshwa zaidi, na kwamba ifikapo mwaka 2018 serikali itanunua ndege nyingine moja na pia mwaka 2019 inatarajia kununua ndege nyingine.
Profesa Mbarawa alitembelea pia karakana iliyopo katika uwanja huo wa ndege na baadaye alitembelea chuo cha mafunzo kwa wafanyakazi wa ndani ya ndege ambako alizungumza na wanafunzi waliokuwepo.
Aliwataka kufanya kazi kwa bidii kwani serikali inajenga ATCL mpya ambayo inatoa huduma bora kwa wateja wake.
“Mmekuja hapa mnaijua ATCL? Hapa tunataka watu wanaotoa huduma nzuri, ile culture (utamaduni) iliyokuwepo nyuma kama mmekuja nayo mjue mlango uko wazi hautachukua miezi sita mtaondoka. Mkifanya kazi hapa mfanye kwa bidii, mkahudumie watu kwa ukarimu kwa sababu tunataka kujenga ATCL mpya ambayo inaongoza ndege zote na hatutamvumilia mtu ambaye anaturudisha nyuma,” alieleza Profesa Mbarawa.
Aliwataka wafanyakazi hao wa ACTL kuachana na mfumo uliopita badala yake kufanya kazi kwa bidii kuijenga ATCL mpya.
Mkurugenzi Mkuu wa ATCL, Ladislaus Matindi alisema kampuni hiyo inaboresha huduma zake ambako kwa sasa wanaboresha huduma za mtandaoni kwa ajili ya watu kushika nafasi ya safari na hata kulipia kupitia mitandao ya simu.

Tuesday, November 15, 2016


DPP amwondolea mashtaka mbunge wa Sumve Mhe Richard Ndassa



Hatimaye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam imemwachia huru Mbunge wa Sumve (CCM),  Richard Ndassa (56) baada ya upande wa Jamhuri kuomba kumuondolea kesi  kushawishi na kuomba  rushwa ya Sh.milioni 30.
 
Ndassa alikuwa anakabiliwa na shtaka la kushawishi na kuomba rushwa kutoka  kwa Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Felichesmi Mramba.
 
Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dennis Lekayo jana aliwasilisha maombi ya kumwondolea Ndassa mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Victoria Nongwa.

Lekayo alidai kuwa Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP), ameona hana nia ya kuendelea na mashtaka yaliyopo mahakamani dhidi ya mshtakiwa chini ya kifungu cha 98 (a) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA).
 
Aidha kwa mujibu wa kifungu hicho kinampa mamlaka DPP ya kumwondolea mashtaka mtuhumiwa kabla ya kusikiliza ushahidi lakini anaweza kukamatwa na kushtakiwa upya.
 
Hakimu Nongwa alisema kwa kuwa upande wa Jamhuri umeomba kumwondolea mshtakiwa mashtaka na kwamba hawana nia ya kuendelea na kesi hiyo, mahakama yake imekubali ombi hilo.
 
"Mahakama hii inamwachia mshtakiwa chini ya kifungu cha 98 (a) kama upande wa Jamhuri ulivyowasilisha maombi yao dhidi ya mshtakiwa" alisema Hakimu Nongwa.
 
Mapema mwaka huu,  Mbunge huyo ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji  ya Umma, alifikishwa mahakamani hapo na kusomewa shtaka la kushawishi na kuomba rushwa ya Sh. milioni 30.
 
Katika kesi ya msingi, Lekayo alidai kuwa Machi 13, mwaka huu, jijini Dar es Salaam,  Ndassa aliomba rushwa Sh.milioni 30 kutoka kwa Mramba.
 
Ilidaiwa kuwa aliomba rushwa ili awashawishi wajumbe wenzake wa kamati hiyo  watowe mapendekezo mazuri  katika mahesabu ya fedha ya Tanesco kwa mwaka wa fedha 2015/2016.
 
Katika shitaka la pili, mwakilishi huyo wa wananchi siku ya tukio la kwanza pia aliomba rushwa ya huduma ya umeme kwa kumshawishi Mramba atowe huduma hiyo kwa ndugu wa mbunge huyo Matanga Mbushi,Richard Ndassa na rafiki wa ndugu yake Lameck Mahewa.
  
Mbunge huyo alikana mashitaka yake na alikuwa nje kwa dhamana.

Tuesday, November 15, 2016

Madini ya Bilioni 3 Yakamatwa Yakitoroshwa



Siku chache baada ya Rais John Magufuli kusema kuna utoroshaji mkubwa wa madini kupitia viwanja vya ndege vilivyopo migodini, Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) umekamata madini yenye thamani ya Sh3,353,421,381.4 yakitoroshwa katika viwanja vikubwa vya ndege na katika matukio 25 tofauti.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa TMAA, Mhandisi Dominic Rwekaza ameeleza hayo katika ripoti ya ukaguzi iliyofanywa na wakala huo mwaka 2015 akisema: “Katika kufuatilia usafirishaji wa madini nje ya nchi katika viwanja vikubwa tulikamata madini yanayotoroshwa yenye thamani ya Dola za Marekani 1,512,186.61 na mengine ya Sh34,670,794 katika matukio 25 tofauti.” 

Akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari nchini hivi karibuni jijini, Rais Magufuli alisema pamoja na kwamba Tanzania ina utajiri mkubwa wa madini, kumekuwa na utoroshwaji wa madini kwa ndege zinazoruka kutoka kwenye baadhi ya migodi.

“Tuna dhahabu ambazo zinachimbwa, lakini utakuta watu wanasafirisha makontena ya mchanga unapelekwa kwenda kusafishwa na sisi ndiyo tunasindikiza na wananchi mpo mnashangilia,” alisema Rais Magufuli.

“Kwa sababu kule wanakwenda ku-separate (kutenganisha). Kwa nini tusijenge separation plant hapa tukatengeneza ajira hapa kwa Watanzania,” alihoji. 

Viwanja vya ndege migodini 
Hata hivyo, wakala huo umesema suala la migodi mikubwa kuwa na viwanja vya ndege kwa ajili ya kusafirishia madini haliepukiki kwa sababu za kiusalama.

Akifafanua ripoti ya ukaguzi wa madini ya mwaka 2015, Msemaji wa TMAA, Isambe Shiwa alisema licha ya kudhibiti utoroshwaji huo viwanja vya ndege vinatumika kusafirishia madini kutoka migodini moja kwa moja kwa sababu za kiusalama.

“Katika maeneo yote ya madini, kuna mawakala wa ukaguzi wa madini, wanashuhudia uzalishaji wa madini, hasa kwa dhahabu wana chukua mikuo (mche wa dhahabu) yake na kuileta kwenye maabara zetu ili ipimwe kujua kiasi cha dhahabu na fedha kisha wanakokotoa mrabaha kulingana na madini husika,” alisema.

“Ili kujua faida ya madini katika mgodi husika, huwa tunafanya ukaguzi yakinifu na kukokotoa kodi zinazotakiwa hasa kodi ya shirika. Kama kuna utata kwenye taarifa za mgodi kuhusu ununuzi wa vifaa na mitambo, tunakagua na kuweka wazi gharama zake kisha tunapeleka TRA kiasi kinachotakiwa kulipwa.”

“Kwa mfano ukiangalia bei ya madini ya dhahabu, kwa wastani gramu moja huuzwa Sh100,000, hivyo kilo moja huuzwa Sh1 bilioni.Ule mkuo mmoja una kilo 20 hadi 25. Unaweza kuviweka vile vipande kwenye mkoba ila ni vizito kubeba. Ukishazalisha hadi mikuo 20 ya dhahabu unabeba mabilioni ya fedha, utasafirishaje kwa gari?

“Kuna wakati pale mgodi wa Geita (GGM) kulikuwa na ndege iliyobeba dhahabu, kumbe tayari watu walishatoa taarifa nje kwa watu waliojitayarisha na silaha za kivita, wakaitungua ilipokuwa ikiruka. Bahati nzuri rubani aliimudu na kufanikiwa kuirudisha uwanjani.”

Alisema kutokana na matukio hayo, sasa wanasafirisha madini kwa helikopta ambayo ikichukua mzigo hupaa kwenda juu zaidi kisha kwenda Dar es Salaam ambako hukaguliwa tena kabla ya kwenda nje ya nchi.

“Kutokana na ukaguzi unaofanyika, naweza kusema hakuna madini wala mchanga unaosafirishwa kwa wizi kwenye migodi yote.Kwanza hii migodi inamilikiwa na wana hisa walioko ndani na nje ya nchi. Wao nao wanataka kupata taarifa za ukaguzi wetu ili wajue wanalipa kodi kiasi gani na wanapata nini,” alisema.

Akizungumzia sababu za madini ya tanzanite kuuzwa zaidi na Kenya, Afrika Kusini na India, Shiwa alisema ni kutokana na Sheria ya Madini ambayo hukata mrabaha wa asilimia tano ya madini hayo wakati sheria ya nchi hizo haina, hivyo kuvutia zaidi wasafirisha madini kupitia nchi hiyo.

“Baada ya kugundua udhaifu huo, kamishna wetu wa madini na ofisa mtendaji wetu mkuu walikwenda Kenya kuzungumza nao ili nao waweke mrabaha huo na kweli waliweka. Hivyo kwa miaka minne iliyopita madini hayo yamepungua sana Kenya,” alisema.

Alisema wamechukua pia hatua ya kuongeza thamani ya madini hayo kwa kuyakata baada ya kujenga viwanda mkoani Arusha hivyo kupunguza usafirishaji wa madini ghafi kupitia Kenya, Afrika Kusini na India. 

Tuesday, November 15, 2016

Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Jumanne ya Novemba 15




Wadaiwa Bodi ya Mikopo wapewa siku 30



BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini imetoa siku 30 kwa wadaiwa sugu ili walipe kiasi chote cha mikopo wanayodaiwa vinginevyo watawachukulia hatua kali watakaokaidi ikiwemo kuwafikisha mahakamani.
Aidha, imesema baada ya kukamilisha taratibu za kuwafikisha mahakamani wadaiwa wote sugu, watawajibika kulipa gharama za kesi na gharama nyingine za kuwatafuta.
Mkurugenzi Mtendaji wa bodi hiyo, Abdul-Razaq Badru amesema jijini Dar es Salaam kuwa, hatua zitachukuliwa kwa wadaiwa wote sugu ambao hawajalipa mikopo yao, licha ya kukumbushwa kwa njia mbalimbali.
Alisema wadaiwa hao walikumbushwa kwa notisi ya Machi mwaka huu, hivyo bodi hiyo imepanga kutangaza tena majina ya wadaiwa hao sugu kwenye vyombo mbalimbali vya habari nchini na kutoa muda wa siku 30 ili walipe kiasi chote cha mikopo wanayodaiwa.
Aidha, alisema watawasilisha majina ya wadaiwa sugu kwenye Wakala wa Kumbukumbu za Mikopo ili yatumike na vyombo vingine vya fedha.
“Bodi ya Mikopo inawataka wadaiwa wote kulipa mikopo yao iliyoiva kabla hatua zaidi hazijachukuliwa. Pia bodi inawashukuru na kuwapongeza wote waliomaliza kulipa mikopo yao na wale wanaoendelea kulipa,” alisema Badru.
Alisema kumbukumbu za bodi zinaonesha kuwa jumla ya wanufaika wa mikopo 93,500 wamebainika na kupelekewa ankara za madeni yao na kati yao wanufaika 81,055 wanalipa mikopo yao na wanufaika wengine 12,445 licha ya kubainika na kupelekewa ankara na madeni yao, hawajaanza kulipa.
Alisema wanufaika 142,470 wenye mikopo iliyoiva yenye jumla ya Sh 239,353,750,176.27 hawajajitokeza na madeni yao ni ya muda mrefu na hivyo kuwafanya kuwa ni wadaiwa sugu.
“Kwa kitendo hicho wanufaika hao wamevunja sheria kama ilivyobainishwa kwenye kifungu cha sheria namba 19A(1) cha Sheria ya Bodi ya Mikopo,” alieleza Badru.
Hata hivyo, alisema kuanzia Julai, 2005 hadi Juni 30, mwaka huu, Bodi ya Mikopo imetoa Sh 2,544,829,218,662.50 kwa jumla ya wanafunzi 330,801 na hivyo kufanya jumla ya fedha zilizokopeshwa tangu mwaka 1994/1995- 2015/2016 kuwa ni Sh 2,595,932,904,575.56 na wanafunzi ni 379,179.
Alisema kati ya mikopo yote iliyotolewa mikopo iliyoiva ni Sh 1,425,782,250,734.31 iliyotolewa kwa wanufaika 238,430 ambao wamemaliza kipindi chao cha matazamio kwa kuwa mikopo hiyo hulipwa kwa kipindi cha kati ya miaka 10 na kuendelea. Hadi kufikia Septemba, 2016 mikopo iliyoiva ni Sh 427,708,285,046.48.



Kimeta chaua nyumbu 90 Monduli

s ZAIDI ya nyumbu 90 na swala 15 wamekufa katika eneo la mapito ya wanyamapori, lililopo kwenye kata ya Selela wilayani Monduli mkoani Arusha.
Inadaiwa kuwa wanyama hao wameangamia kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa kimeta ulioibuka katika ushoroba huo wa Selela, unaoziunganisha mbuga za Tarangire na Hifadhi ya Ziwa Manyara, pia umeangamiza idadi kubwa ya wanyama wa kufugwa hasa ng'ombe, mbuzi na kondoo wapatao 60, huku idadi ya vifo ikitarajiwa kuongezeka.
Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Idd Kimanta amesema baada ya matukio ya wanyamapori kuanguka ghafla na kufa kwa wingi na baadaye mifugo pia kuanza kuangamia, uongozi wa wilaya ulipeleka sampuli za mizoga hiyo kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwa ajili ya uchunguzi na ambaye alithibitisha uwepo wa kimeta.
“Tunahofia kuwa kimeta sasa kitakuwa kimesambaa maana wanyama kama nyumbu wana tabia ya kuhamahama kutoka sehemu moja hadi nyingine, hivyo si ajabu wamepeleka ugonjwa huu maeneo mengine," alisema.
Ofisa Mifugo wilayani Monduli, Salum Omar amethibitisha kufa kwa ng'ombe, mbuzi na kondoo kadhaa katika eneo lake na kuongeza kuwa hivi sasa wameanza taratibu za kutoa chanjo dhidi ya maambukizi ya kimeta kwa mifugo iliyobaki.
“Lakini kuna haja pia ya kuhakikisha kuwa wafugaji, wengi wakiwa ni wa jamii za Kimasai, wanapewa elimu juu ya mlipuko wa ugonjwa huu, maana wengi wanakula mizoga ya mifugo yao iliyokufa,” alionya ofisa mifugo huyo.
Kwa kawaida binadamu akigusa mzoga wa mnyama aliyekufa kwa kimeta, huweza kupata maambukizo hayo. Sasa wafugaji wa Monduli wanakwenda mbali zaidi, kula nyama iliyoathirika.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Selela, Julius Loiboseki ameomba msaada kwa serikali iwasaidie kuzuia mifugo kutoka maeneo ya jirani ili isiingizwe kwenye maeneo yao hadi pale tatizo litakapotatuliwa.
Kauli hiyo imeungwa mkono na Diwani wa Kata hiyo ya Selela, Cuthbert Meela ambaye alifafanua kuwa wilaya ya Monduli haijawahi kukumbwa na mlipuko wa kimeta au ugonjwa wowote ule mkubwa wa kutishia maisha ya watu na wanyama.



Viwanda 1,845 vyaanzishwa mwaka mmoja



KATIKA kipindi cha mwaka mmoja kilichoanzia Novemba mwaka jana mpaka Oktoba mwaka huu ambacho kimeongozwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini Rais John Magufuli, jumla ya viwanda vipya 1,845 vimeanzishwa na hivyo kufanya jumla ya viwanda vyote nchini kufikia 54,422.
Hayo yalibainishwa hivi karibuni mjini Dodoma na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati akiahirisha Mkutano wa Tano wa Bunge la 11.
Waziri Mkuu Majaliwa alifafanua kuwa kwa mujibu wa ripoti iliyotokana na sensa ya viwanda iliyofanyika kuanzia mwaka 2013/14 hadi mwaka jana ilionekana kuwa mpaka Oktoba mwaka jana kulikuwa na viwanda 52,579.
“Ni matumaini ya Serikali kuwa kutokana na juhudi za uhamasishaji zinazofanyika, kasi ya uanzishwaji viwanda na hasa viwanda vidogo na vya kati na vikubwa itaongezeka sana,” alisisitiza Majaliwa katika hotuba hiyo ambayo hata hivyo hakuisoma bungeni kutokana na msiba wa Mbunge wa Dimani, Hafidh Ali Tahir, badala yake ikawekwa katika kumbukumbu rasmi za Bunge.
Alisema katika matokeo ya sensa hiyo hadi kufikia mwaka 2013, Tanzania ilikuwa na jumla ya viwanda 49,243 ambapo viwanda vidogo vinavyoajiri mtu mmoja hadi wanne vilikuwa ni asilimia 85.13 na viwanda vidogo vyenye watu watano hadi 49 vilikuwa asilimia 14.02.
Alisema matokeo hayo pia yalionesha kuwa viwanda vya kati vyenye watu 50 hadi 90 vilikuwa ni asilimia 0.35 na viwanda vikubwa vyenye watu kuanzia 100 na kuendelea ni asilimia 0.5.
Hivyo, Asilimia 99.15 ya viwanda vyote nchini ni viwanda vidogo.
Alisema serikali kupitia wizara mbalimbali za kisekta tayari imebainisha maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya kuchochea uwekezaji kama vile kuendeleza eneo la mji wa Kigamboni na kutenga maeneo maalumu ya uwekezaji katika mikoa mbalimbali nchini.
“Hatua nyingine ni kuboresha miundombinu kama vile barabara na reli. Mfano mzuri ni ujenzi wa reli yenye urefu wa kilomita nne katika kiwanda kipya cha Kilua Group cha kutengeneza nondo kilichopo Mlandizi, Pwani,” alisema Waziri Mkuu Majaliwa.
Waziri Mkuu alifafanua kuwa serikali inaendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa viwanda mbalimbali nchini na kwa viwanda vilivyopo karibu na bomba la gesi vitaunganishwa na bomba hilo ili vitumie gesi. Aidha, alisema tayari serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha kasi ya uwekezaji kwenye sekta ya viwanda inaongezeka ili ichangie asilimia 15 ya Pato la Taifa ifikapo mwaka 2020.
Alitaja baadhi ya mikakati hiyo kuwa ni kutambua sekta za kipaumbele kwa kuzingatia viwanda vinavyotumia malighafi za ndani, hususan kwenye sekta za kilimo na maliasili ili kuchochea uzalishaji vijiini na kuongeza ajira; kuandaa mpango mahsusi wa uwekezaji kwenye viwanda kupitia mifuko ya hifadhi ya jamii na kuhamasisha sekta binafsi, ya ndani na nje ya nchi, kuwekeza kwenye viwanda.
Alisema pia mkakati mwingine ni kutoa elimu na mwongozo kwa serikali ngazi ya mikoa na wilaya kuendelea kuhamasisha uwekezaji katika maeneo yao.

Reviewed by RICH VOICE on Novemba 14, 2016 Rating: 5

Hakuna maoni

Chapisho Lililoangaziwa

Thursday, September 15, 2016 Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Alhamisi Ya Septemba 15 ...