Monday, November 14, 2016

Wadaiwa Sugu Bodi ya Mikopo wapewa siku 30



Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi Mtendaji wa bodi hiyo Abdul-Razaq Badru amesema kuwa hadi sasa kuna jumla ya wadaiwa sugu 142,470 wenye mikopo ya shilingi 239,353,750,170.27 iliyokwishaiva hawajajitokeza wala kuanza kulipa mikopo yao.

Akitolea ufafanuzi wa maana ya neo "Wadaiwa Sugu", Badru amesema kuwa ni wanufaika waliokopeshwa, muda wa matarajio ukapita bila kuwasilisha taarifa zao na kulipa madeni ya mikopo waliyokopeshwa tangu mwaka wa masomo 1994/1995.

Kuhusu hatua zinazochukuliwa na bodi hiyo, Badru amesema mbali na kutoa siku 30, bodi hiyo inakamilisha taratibu za kuwafikisha mahakamani kwa kuvunja sheria ya bodi ya mikopo kifungu cha 19A(1).

Hatua nyingine ni pamoja na kuyawasilisha majina hayo katika taasisi za mikopo, kuwasiliana na wadhamini wao pamoja na kuyatangaza hadharani majina ya wadaiwa sugu wote ili waajiri, wadhamini na wadau wengine wayajue na kutoa taarifa katika bodi hiyo.

Kuhusu takwimu za mikopo iliyotolewa, amesema tangu 1994/95 hadi 2015/16 jumla ya shilingi 2,595,932,575.56 zimekopeshwa kwa jumla ya wanufaika 379,179.

Amesema kati ya mikopo yote iliyokopeshwa, mikopo iliyoiva ni shilingi 1,425,708,285,046.48 kwa wanufaika 238,430 ambao tayari wamemaliza kipindi chao cha matazamio.

Badru amesema kuwa jumla ya wanufaika wa mikopo 93,500 wamebainika na kupelekewa ankara za madeni yao, ambapo kati yao wanufaika 81,055 wanaendelea kulipa.
 
 

Monday, November 14, 2016

ACT-Wazalendo walaani kauli ya Serikali kutowajengea wananchi......Wadai kauli hiyo ni fedheha kwa waathirika na Wadau.


Watanzania wanakumbuka kuwa mnamo tarehe 10 Septemba, 2016 lilitokea tetemeko la ardhi katika eneo la Kanda ya Ziwa na hususan Mkoa wa Kagera.

Tetemeko hilo lilisababisha athari mbalimbali zikiwemo vifo, majeruhi, uharibifu wa makazi na miundombinu ya umma na watu binafsi. Jumla ya Watu 117,721 wameathirika kwa kupoteza makazi yao, mali na athari za kisaikolojia katika Wilaya za Bukoba, Missenyi, Muleba, Karagwe na Kyerwa.

Aidha, jumla ya watu 17 walipoteza maisha na 560 walijeruhiwa. Vilevile, nyumba 2,072 za makazi zilianguka kabisa na nyumba 14,595 za makazi zilibomoka, baadhi zina kuta au kupata nyufa kubwa na hivyo kuzifanya kuwa hatarishi kwa makazi ya binadamu. Vilevile, maafa haya yalisababisha uharibifu mbalimbali wa miundombinu ya barabara na majengo ya watu na taasisi mbalimbali, ikiwemo shule na Hospitali.

Kufuatia maafa hayo, wananchi na taasisi mbalimbali, pamoja na nchi marafiki, waliitikia wito wa kuwasaidia wahanga wa maafa na kukarabati miundo mbinu iliyoharibika. Hadi kufikia mwezi Oktoba, Fedha, Vyakula na Vifaa mbalimbali vya Ujenzi vilikuwa vimepatikana kwa njia ya michango mbalimbali.

Chama chetu kimeshtushwa na kauli ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera kwamba Wananchi walioathirika wajitegemee wenyewe na kwamba misaada yote iliyotolewa Ni ya Serikali na Taasisi zake tu. Kauli hii ya Mkuu wa Mkoa haikubaliki kwani inadhalilisha waathirika na watu wote waliojitoa kuwasaidia waathirika hao.

Tunachukulia kauli hii kama tangazo la wizi wa uaminifu wa wananchi waliochanga. Ni busara ya kawaida kuwa hatua ya kwanza katika kushughulikia maafa ni kurudisha hali ya maisha ya watu katika hali ya kawaida sambamba na ukarabati wa miundombinu. Aidha, suala la ujenzi wa miundo mbinu ya taasisi za umma ni jukumu la msingi la serikali. Kwa sababu hii:

• ACT Wazalendo tunaitaka serikali kuu kujitenga na kufuta kauli ya mkuu wa mkoa wa Kagera kwa sababu inaigombanisha serikali na wananchi inaowaongoza.

• ACT Wazalendo tunaitaka serikali kuelekeza ni misaada iliyopatikana kwa michango ya wananchi, taasisi na nchi rafiki katika kusaidia wananchi walioathirika kurudi katika maisha ya kawaida, ikiwemo ukarabati na ujenzi wa nyumba za kuishi.

• ACT Wazalendo tunatoa wito kwa taasisi za kiraia nchini kuchukua nafasi yake katika kuendelea kuikumbusha serikali wajibu wake wa msingi wa kuboresha maisha ya watu.

Janeth Rithe
Katibu wa Taifa ACT Wazalendo, Kamati ya Maendeleo ya Jamii
13/11/2016, Dar Es salaam.
 
 

Monday, November 14, 2016

Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS ) amtaka Rais Shein asisaini muswada wa mafuta na gesi


Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS ), Omar Said Shaaban amemshauri Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein asiusaini Muswada wa sheria ya mafuta na gesi uliopitishwa na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi hivi karibuni kwa madai kuwa unavunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano.

Omari ameeleza msimamo huo katika barua yake ya maneno 1,293 aliyomwandikia Dk Shein akifafanua jinsi gani muswada huo unavunja sheria na Rais huyo anavyoingizwa kwenye mtego wa kuvunja Katiba.

Katika barua hiyo, mwanasheria hiyo anasema, “Mheshimiwa Rais, zipo taarifa kuwa unajiandaa kuweka saini kwenye muswada huo uliopitishwa na Baraza la Wawakilishi ili hatimaye iwe sheria. Naomba nikunasihi uachane na mpango huo ili kujiepusha na mtego wa jaribio la kuvunja Katiba.”

Anasisitiza, “Kwa heshima naomba nikueleze kuwa jaribio la Serikali yako na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar na hatua yako ya kuweka saini muswada huo ili uwe sheria, ni uvunjaji mkubwa wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo wewe umeapa kuilinda, lakini pia ni kinyume na maelekezo ya sheria inayorejewa kama ndiyo chanzo cha mamlaka ya Zanzibar kutunga sheria yake.”

Mwanasheria huyo anabainisha kuwa kama kweli nia ya dhati ipo ya kuondoa mafuta na gesi kwenye Muungano, hatua pekee na salama kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kusukuma kumalizika kwa mchakato wa Katiba Mpya au kupelekwa mabadiliko ya Katiba Bungeni kuliondoa jambo hilo kwenye Nyongeza ya Kwanza ya Katiba.

Omari alisema akiwa mwanasheria tena kiongozi kwenye kada hiyo, ana wajibu wa kikatiba, kimamlaka na kitaaluma kusimamia ulindwaji na usimamizi wa Katiba na sheria za nchi na akiwa mwenye uchungu na Zanzibar, anapenda kuona ikisimamia rasilimali zake yenyewe bila ya kukiuka masharti ya Katiba.

Alibainisha kuwa katika Katiba ya Muungano kwenye nyongeza ya kwanza, suala la mafuta na gesi ni jambo la Muungano hivyo usimamizi wake na utungiwaji sheria kwa mujibu wa Katiba zote mbili upo chini ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 “Hakuna mahali duniani kote ambapo suala lenye misingi yake kikatiba linaondolewa kwa “makubaliano ya viongozi wa wakuu wa Serikali,” anasema. 
 
 

Monday, November 14, 2016

Donald Trump Akataa Kulipwa Mshahara wa Urais


Rais mteule wa Marekani, bilionea Donald Trump amesema hatakubali kupokea mshahara wa urais pindi atakapokuwa madarakani.

Trump ameweka msimamo huo jana katika mahojiano maalum na mtangazaji maarufu, Lesley Stahl katika kipindi cha 60 Minutes, aliyetaka kufahamu kuhusu uamuzi wake juu ya mshahara wake akiwa ni mfanyabiashara mkubwa.

“Sijawahi kuzungumzia hili, lakini jibu langu ni hapana,” alisema. “Nafikiri inanibidi kupokea kwa mujibu wa sheria $1, kwahiyo ntachukua $1 (Sawa na shilingi 2,200 za Tanzania) kwa mwaka. Lakini hata sijui ni nini,” aliongeza.

Ingawa mtangazaji huyo alimkumbusha Trump kuwa anaiacha $400,000 kwa mwaka, rais huyo mteule alisisitiza, “sitachukua mshahara. Sitapokea.”

Wakati wa kampeni, Trump aliahidi kuwa atajiweka kando na biashara zake endapo atachaguliwa kuwa Rais wa Marekani, na kwamba atajikita zaidi katika kutimiza ahadi zake kwa Wamarekani. Alisema kuwa biashara zake ataziacha mikononi mwa watoto wake.
 

Monday, November 14, 2016

Habari Zilizopo Katika Magazeti ya Leo Jumatatu ya Novemba 14



Monday, November 14, 2016

Vyoo 100 kujengwa barabara ya Mwanza Kwenda Dar Es Salaam


Taasisi  ya The Desk & Chair Foundation (TD& CF), inatarajia kujenga vyoo 100 katika Barabara Kuu ya Mwanza-Shinyanga-Dar es Salaam unaokadiriwa kutumia Sh. milioni 500.

Mwenyekiti wa TD & CF, Alhaji Sibtain Meghjee alisema hivi karibuni mjini Mwanza kwamba mradi huo ni sehemu ya miradi mitatu mikubwa ambayo taasisi yake inatekeleza nchini.

Alisema baada ya kukamilisha mradi mkubwa wa  jengo la kupumzikia wananchi wanaokwenda kutibiwa na kuwajulia hali wagonjwa waliolazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza, Sekou Toure wanatarajia kujenga vyoo 100 kwenye barabara ya kutoka Mwanza hadi  Dar es Salaam kwa basi.

Meghjee alieleza kuwa maandalizi ya awali ya mradi huo yameshaanza na kwamba watashirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) ili kupata taarifa sahihi kabla ya mradi kuanza.

“Penye nia pana njia, baada ya kukamilisha ndoto yetu, leo ya mradi huu mkubwa wa ujenzi wa jengo la kupumzikia hapa Sekou Toure, tunatarajiwa kutekeleza miradi mitatu mikubwa ukiwemo wa vyoo  kwa ajili ya abiria wanaosafiri kati ya Mwanza na Dar es Salaam:

“Tunataka msamiati wa kuchimba dawa wakati wa safari ubaki kuwa historia kwa hiyo tunatarajia kufanya jaribio moja la kujenga matundu 100 ya vyoo katika njia na barabara kuu ya Mwanza hadi Dar es salaam ambavyo vitagharimu shilingi milioni 500.Tutashirikiana na mamlaka husika, ofisi yako na idara ya afya,”alisema Meghjee.

Meghjee alieleza kuwa taasisi hiyo pia ina mpango wa kutekeleza mradi wa kutengeneza viungo bandia kwa kushirikiana na kitengo cha Jairpur Foot/Knee and Limb Project cha India ambao unahitaji Dola 200,000 za Marekani (sh. milioni 44), zitakazowezesha kuanzisha huduma ya viungo hivyo bandia vya miguu, mikono, fimbo na baiskeli.

Alisema wanaendelea kuwasiliana na wafadhili watakaoshirikiana nao kwenye mradi huo na kuwahakikishia walengwa kuwa viungo hivyo vitapatikana kwa gharama nafuu mara utakapokamilika mradi huo.

Meghjee aliongeza kuwa wakati wakiendesha ujenzi wa jengo la mapumziko katika Hospitali ya Sekou Toure,walipata wazo la kujenga mabanda yatakayotumiwa na madereva wa pikipiki (boda boda) kuegesha vyombo vyao kivulini na kupata huduma ya vyoo na mabafu.

Mwenyekiti huyo wa TD & CF aliongeza zaidi kuwa endapo Halmashauri ya Jiji itaridhia na kuwapa eneo maalumu na mahususi la ujenzi wa huduma hiyo watafanya jaribio hilo moja ili kuweza kuona matunda yake.
 
 

Monday, November 14, 2016

Kesi ya Akina Zombe: Mrakibu wa Polisi (SP) Bageni Apinga Hukumu ya Kunyongwa Hadi Kufa




Aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kinondoni, Mrakibu wa Polisi (SP),Christopher Bageni amewasilisha maombi Mahakama ya Rufaa ya Tanzania kupinga adhabu ya kunyongwa hadi kufa.

SP Bageni alihukumiwa adhabu hiyo baada ya mahakama hiyo kujiridhisha kwamba aliwaua kwa kukusudia wafanyabiashara wanne wa madini kutoka Mahenge mkoani Morogoro na dereva teksi mkazi wa Manzese, Dar es Salaam,  katika Msitu wa Pande.

Bageni kupitia Wakili wake, Gaudioz Ishengoma,  aliwasilisha maombi hayo mwishoni mwa wiki yaliyoambatana na hati ya kiapo iliyoapwa na wakili huyo.

Muwasilisha maombi anaomba mahakama hiyo kuifanyia marejeo hukumu dhidi yake iliyotolewa Septemba 13 na kusomwa  Septemba 16 mwaka huu na Msajili wa Mahakama hiyo, John Kahyoza.

Akitoa sababu kuomba marejeo, anadai  alinyimwa haki sawa ya kusikilizwa wakati wa kutathmini ushahidi ulioko kwenye kumbukumbu za mahakama kwa kuegemea kwenye ushahidi wa upande wa mashtaka.

Alidai katika kuchanganua ushahidi ambao uamuzi wa mahakama uliegemea, mahakama ilishughulika na ushahidi wa msingi (Exam in Chief) wa upande wa mashtaka na iliangalia kwa juu juu tu ushahidi wa utetezi hususan wa Bageni au haikuutazama kabisa.

“Kuna kukinzana kwa haki kwa maana ya kwamba mtoa maombi alinyimwa haki sawa ya kusikilizwa, kwa mahakama kuchagua na kuegemea   upande wa mashtaka pekee na kushindwa kuzingatia ushahidi wa upande wa utetezi, hasa wa mtoa maombi.

“Uamuzi wa mahakama umetolewa katika msingi wa makosa ya dhahiri kwenye kumbukumbu za mahakama, hivyo kusababisha upotoshaji wa haki, kushindwa kuzingatia mwongozo wa kanuni katika asili, thamani na matumizi ya ushahidi wa kuungwa mkono,” ilisema sehemu ya maombi hayo.

Alidai kuwa kwa kushindwa kuchanganua na kutathmini  ushahidi kwa umakini kwenye kumbukumbu, mahakama ilishindwa kuainisha ushahidi wa mjibu rufaa wa nne (Bageni)  kimazingira kama ilivyo ni dhahiri unakosa thamani ya kuhitaji ushahidi wa kuunga mkono na hivyo si salama kuegemea katika kumtia hatiani.

“Kwa kushindwa kuona na kuzingatia ushahidi uliokusudiwa kuwa na ushahidi wa kuunga mkono, siyo ushahidi huru na hauna mashiko kuthibitishwa (PW27) na haupo (PW36).

“Kwa kushindwa kufanya uchambuzi wa ushahidi kwenye kumbukumbu kwa umakini wenye manufaa, vinginevyo mahakama ilipaswa kuona wajibu wa kuthibitisha shtaka kwenye jinai haukufikiwa,”anasema Wakili Ishengoma.

Anadai mahakama katika kuamua, kama ilivyofanya katika uhalisia wake, kuhusu ushiriki wa mtoa maombi katika eneo la tukio la uhalifu, ilishindwa kubaini katika ujumla wake ushahidi wa upande wa mashtaka ambao haukuweza kuthibitisha mashtaka bila kuacha shaka.

Ishengoma alidai mahakama haikuuchukulia ushahidi kwenye kumbukumbu katika ujumla wake hivyo kutengua uamuzi wa kuachiwa huru kwa mtoa maombi na kumtia hatiani na kuhukumiwa adhabu ya kifo kwa kusimamia ushahidi ambao haupo na uvumi pamoja na ushahidi wa mashaka makubwa.

Alidai kutokana na hukumu ya mahakama, haikuwa bayana ni kwa ushahidi wa nani ulithibisha mtoa maombi Bageni alimwezesha au kumsaidia nani katika mauaji ya marehemu hao.

Katika hati ya kiapo iliyoapwa na Wakili Ishengoma, Bageni anadai yeye na wengine wanane ambao hawako katika maombi hayo walishtakiwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kwa makosa ya mauaji ya watu wanne katika Kesi ya jinai namba 26 ya mwaka 2006.

Bageni alikuwa mshtakiwa wa pili na katika hukumu iliyotolewa na Jaji Salum Massati, amnayo  wote waliachiwa huru, lakini Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) hakuridhishwa na uamuzi huo hivyo alikata rufaa namba 358 ya mwaka 2013.

Kabla ya usikilizwaji wa rufaa hiyo, DPP aliwaondolea rufaa wajibu rufaa watano na kubaki wajibu rufani wanne ambao waliachiwa huru pia Septemba 16, mwaka huu.

Walioachiwa huru ni aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam (RCO) Kamishna Msaidizi wa Polisi Abdallah Zombe na maofisa wengine wawili baada ya mahakama kuona hakuna ushahidi wa wazi ama mazingira kuwatia hatiani.

Katika kesi ya msingi, Bageni alidaiwa kuwaua kwa kukusudia wafanyabiashara Sabinus Chigumbi, maarufu Jongo na ndugu yake, Ephrahim Chigumbi, Mathias Lunkombe na Juma Ndugu, aliyekuwa dereva wa teksi wa Manzese , Januari 14, mwaka 2006, katika Msitu wa Pande, Mbezi Luis, Dar es Salaam.
 
 

Monday, November 14, 2016

Kidato cha Pili Waanza Mitihani leo


Wanafunzi wa kidato cha pili nchini wameanza kufanya mitihani yao ya upimaji leo katika shule za sekondari 4,669 zilizopo Tanzania Bara.

Jumla ya wanafunzi 435,221 wamesajiliwa kufanya mitihani hiyo wakiwamo 67 wasioona na 306 wenye uoni hafifu.

Mbali na mitihani hiyo, Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Taifa (Necta), Dk Charles Msonde amesema mtihani wa Taifa wa darasa la nne utafanyika Novemba 23 na 24, mwaka huu.

"Mitihani hii inafanyika katikati ya mafunzo ili kubaini changamoto zilizopo na kutafuta namna ya kuboresha mafunzo hayo," amesema Dk Msonde.                      

Wakati huo huo, Dk Msonde amefafanua kuwa mafunzo ya ualimu wa shule ya msingi ngazi ya stashahada yamefutwa lakini wanafunzi waliopo vyuoni watamalizia masomo yao kwa muda uliobaki.

Dk Msonde amesema mafunzo hayo ya walimu yataendelea kwa utaratibu wa zamani ambao ulikuwa ngazi ya cheti.

Amesema usimamizi wa mitihani hiyo itakuwa chini ya Necta kama ilivyokuwa zamani badala ya Nacte.

"Wanafunzi walio vyuoni wataendelea na mafunzo hayo, isipokuwa kuanzia mwaka huu hatutadahili kwa ngazi ya diploma, tutadahili ngazi ya cheti kama ilivyokuwa zamani," amesema Dk Msonde.
Reviewed by RICH VOICE on Novemba 14, 2016 Rating: 5

Hakuna maoni

Chapisho Lililoangaziwa

Thursday, September 15, 2016 Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Alhamisi Ya Septemba 15 ...