HABARI ZA ALHAMISI HII

Thursday, October 27, 2016

TFS Yanasa Lori Likisafirisha Mbao Kinyume cha Sheria

SeeBait

______________________
Kikosi cha Kufuatilia na Kuzuia Uharibifu wa Misitu cha Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kwa kushirikiana na Kikosi Dhidi ya Ujangili kanda ya Dar es Salaam kimefanikiwa kukamata lori lenye namba za usajili T 676 ANQ lililokuwa likisafirisha mbao kinyume cha sheria huku zikiwa zimefichwa kwa kufunikwa na bidhaa mbalimbali ikiwemo sabuni ili zisionekane kiurahisi kwenye vituo vya ukaguzi.

Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam leo, Kaimu Afisa Habari wa Wakala huyo, Nurdin Chamuya alisema tukio hilo limetokea tarehe 14 Oktoba, 2016 majira ya saa kumi usiku maeneo ya Amana, Ilala Jijini Dar es Salaam baada ya kupata taarifa kutoka kwa raia wema juu ya uwepo lori hilo katika maeneo hayo.

Chamuya alisema baada ya kupata taarifa hizo vikosi hivyo vilifika eneo la tukio na kufanya mahojiano na baadhi ya wananchi waliokuwa karibu na lori hilo ambapo mmoja kati ya wahudumu wa lori hilo alieleza kuwa lori hilo lilitokea Mkoani Kigoma na kwamba lilikuwa limepakia mzigo wa sabuni na chupa za maji zilizotumika. Dereva wa lori hilo hakuweza kupatikana.

“Wahudumu hao walipotakiwa kufungua mlango wa lori hilo kwa ajili ya upekuzi zaidi walisita kwa madai kuwa hawakuwa na funguo za lori hilo, Hatimaye   waliwasiliana na mmlikiwa wa eneo ambaye alikuwa amekabidhiwa funguo kwa ajili ya ulinzi” alisema Chamuya.

Alieleza kuwa mmiliki huyo alipofika alisema, anamfahamu mwenye gari ambaye ndiye mpangaji wa eneo lilipokutwa gari na kwamba anazo taarifa za  gari hilo,  na ameombwa apokee mzigo na kuutunza hadi atakaporudi kutoka safari ya  Mwanza kwa tatizo la msiba wa Baba yake.

Baada ya mmiliki wa eneo hilo kufanya mawasiliano na mwenye gari kuhusu mzigo uliokuwa kwenye gari hilo, mwenye gari alieleza kuwa kwa taarifa za dereva wake na ajenti aliyepakia mzigo Kigoma, gari lake lilikuwa na chupa chakavu na sabuni kutoka Kigoma na hakuna aina nyingine ya mzigo kwa ufahamu wake na akaruhusu gari hilo kufunguliwa mbele ya mwenye eneo.

“Baada ya gari hilo kufunguliwa, kilichoonekana kwa urahisi ni sabuni na mifuko michache inayosomeka kwa nje kuwa ni dawa ya kuku. Baada ya upekuzi ndipo zilionekana mbao zilizokuwa zimefichwa chini ya katoni za sabuni. Tumeshikilia Lori hilo kwa hatua zaidi za kisheria.

“Kufuatia tukio hili, Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania tunatoa onyo kali kwa wale wote wanaojihusisha na vitendo vya uvunaji na usafirishaji wa mazao ya misitu kinyume cha sheria ya misitu namba 14 ya mwaka 2002 pamoja na kanuni zake za mwaka 2004 na kwamba watakaobainika watachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria za nchi” alisema Chamuya.

Akizungumzia athari mbalimbali za vitendo hivyo vya uvunaji holela wa mazao ya misitu bila ya kufuata taratibu za kisheria za uvunaji endelevu alisema vitendo hivyo vinatishia nchi kuwa jangwa ambapo takwimu zinaonyesha jumla ya hekta 372,000 za misitu nchini hupotea kila mwaka kutokana na matumizi makubwa ya rasilimali hizo ambayo yanazidi uzalishaji wake kwa ujazo wa mita 19.5 milioni kwa mwaka.

Chamuya ametoa wito kwa wananchi wote nchini kushirikiana na Serikali katika uhifadhi na ulinzi wa rasilimali za misitu na kuacha fikra potofu kuwa kazi hiyo ni ya Serikali pekee na taasisi zake kwakuwa faida zake hunufaisha jamii yote na vivyo hivyo kama athari zitajitokeza basi zitaikumba jamii yote bila kubagua.

Thursday, October 27, 2016

Serikali Yatangaza Matokeo ya Mtihani Darasa la 7......Bofya hapa Kuyaona

SeeBait

Serikali  imetangaza  matokeo  ya  mtihani  wa  darasa  la  7 kwa mwaka 2016  ambapo ufaulu  umeongezeka  kwa asilimia 2.52 na shule iliyoongoza kitaifa ni shule ya Msingi Kwema  ya  mkoani Shinyanga


AU 

 

Thursday, October 27, 2016

Sakata la posho za madiwani Arusha laibukia bungeni

SeeBait
Sakata la posho za madiwani wa Jiji la Arusha bado halijapoa, baada ya Mbunge wa Rombo (Chadema), Joseph Selasini kuliibulia katika Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), akisema linakwamisha ukusanyaji wa mapato. 

Sakata hilo liliibuka jana wakati kamati hiyo ilipokuwa ikipitia na kuhoji hesabu za halmashauri hiyo kwa mwaka wa fedha 2014/2015. 

Mbunge huyo alisema halmashauri hiyo imekata posho kwa madiwani na watendaji na kuzipeleka fedha hizo kwa walimu, jambo ambalo linawavunja moyo wawakilishi hao wa wananchi kutimiza majukumu yao. 

“Madiwani ndiyo wanawasaidia kuwahamasisha wananchi katika ukusanyaji wa mapato na hao mnawavunja moyo. Mkurugenzi hamuwezi kufikia malengo kama mtakuwa watendaji peke yenu,” alisema Selasini. 

Alisema halmashauri hiyo ikimaliza mvutano huo inaweza kuongeza mapato kutoka Sh12 bilioni hadi Sh18 bilioni na kujiendesha bila kutegemea ruzuku. 

Mbunge huyo alisema katika halmashauri zote nchini hakuna diwani anayelipwa posho ya Sh10,000, kwa nini madiwani wa jiji hilo pekee walipwe kiasi hicho. 

Akijibu hoja hiyo, mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Athuman Kihamia alisema hakuna diwani anayelipwa kiasi hicho cha fedha na kwamba, madiwani wote wanalipwa posho ya Sh40,000 kwa mwezi na nauli Sh10,000 kulingana na kanuni walizokubaliana mwaka 2003. 

Alisema madiwani hao walikuwa na posho zipatazo tano ambazo ni nauli, kujikimu, vikao, madaraka na mawasiliano.
Pia, Kihamia alisema walikuwa wakilipwa Sh150,000 za mafuta kinyume na kanuni walizokubali kuzitumia za mwaka huo. 

“Siwezi kurudia makosa kwa kulipa fedha zisizofuata kanuni na utaratibu, maana mtakuja kunihoji hapa kwa nini nimezilipa,” alisema. 

Mbunge wa Kwela (CCM), Ignas Malocha alimpongeza mkurugenzi huyo kwa kufuata misingi na utaratibu wa kanuni na sheria katika uendeshaji wa jiji hilo.

 Akizungumza nje ya kamati hiyo, Meya wa jiji hilo, Calist Lazaro alitaka liachwe lijiendeshe lenyewe bila kuingiliwa. 
 
 

Thursday, October 27, 2016

Madudu Kibao Yaibuliwa Mradi wa NSSF Kigamboni

SeeBait

Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) limekiri kuwapo ubadhirifu kwenye mkataba wa ubia na Kampuni ya Azimio Housing Estates iliyotakiwa kuendeleza ekari 20,000 za ardhi Kigamboni na kuna hatari ya kupoteza Sh bilioni 270.

NSSF pia imekiri ubadhirifu katika utoaji mikopo kwenye Saccos mbalimbali nchini ikiwamo ya Bumbuli, inayoonekana kukopeshwa zaidi ya Sh bilioni mbili, bila kuwa na sifa huku kukiwa pia hakuna kumbukumbu ya mwaka mzima kama walirudisha mkopo wa awali.

Mwenyekiti wa Bodi ya NSSF, Profesa Samuel Wangwe alieleza jana mbele ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kwamba Bodi yake ilipoingia madarakani iligundua ubovu wa mkataba huo na kusitisha kutoa fedha na sasa inaangalia namna ya kujitoa bila kupoteza fedha zilizowekezwa.

Alisema uwekezaji huo ambao ardhi ya mwekezaji ilipaswa kuwa ekari 20,000, hatua ya awali ulipaswa kuanza na ekari 300, lakini uchunguzi uliofanyika hivi karibuni ulionesha kuwa kuna ekari 3,500 pekee hali inayoonesha udanganyifu uliofanyika tangu awali.

Pia mwekezaji huyo alidanganya uhalisia wa bei ya ardhi hiyo, kwani alionesha kuwa thamani ya ekari ya moja ni Sh milioni 800 wakati kiuhalisia, ardhi hiyo thamani yake ni Sh milioni 25 peke yake.

Mwenyekiti wa PAC, Naghenjwa Kaboyoka alisema imekuwa vigumu kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG)  kuthibitisha uwepo wa viwanja hivyo kwa kukosekana hatimiliki, umiliki wa ekari 19,700 za ardhi ambazo ni sehemu ya mtaji wa Azimio Housing Estates kwa asilimia 20, hivyo fedha za NSSF zinakuwa kwenye hatari ya kupotea.

Alisema NSSF ambayo inamiliki hisa ndogo kuliko Azimio, imewekeza fedha nyingi, zaidi ya dola milioni 129 za Marekani wakati mbia huyo aliwekeza dola milioni 5.5.

Akijibu hoja za Mwenyekiti huyo, Profesa Wangwe alisema mradi huo   ulisimama tangu Februari kutokana na mbia kukosa fedha na kwamba hakopesheki kwani NSSF inamdai.

Mbunge wa Msalala, Ezekiel Maige alisema mradi huo wa Kigamboni ni mchafu na katika mazingira hayo ambayo Bodi pia imeshituka kuwa   mchafu hivyo ni vema NSSF ingejitoa kuliko kuendelea na mkataba mbovu.

“Ni vema ukishagundua kuwa unachezea kitenesi kichafu ambacho kilianza kuchezewa na watu ambao wameshaondolewa, usiendelee kucheza na mtu yule yule ili asije kukuingiza katika matatizo makubwa zaidi,” alisema Maige.

Profesa Wangwe alisema ni vigumu kujitoa haraka kwenye mkataba huo, kutokana na fedha nyingi waliyowekeza ambayo iko hatarini kupotea na kwamba ardhi yote ni ya mwekezaji huyo hivyo wanatafuta namna ya kurudisha fedha waliyowekeza hata kama haitakuwa na faida.

Mbunge wa Sumbawanga Mjini, Aesh Hilaly alihoji kama mkataba unaruhusu mwekezaji huyo kukopa ili kuendeleza mradi huo.

Mkurugenzi wa NSSF, Profesa Godius Kahyarara alisema mwekezaji huyo alitaka kukopa NSSF ili aendeleze mradi huo ambao umesimama lakini hakopesheki kwa kuwa anadaiwa.

Hata hivyo, baadhi ya wabunge walihoji uhalali wa Saccos kukopeshwa mara mbili kwa mwaka, huku zingine zikikosa mikopo na vigezo vilivyotukia katika kutoa mikopo hiyo.

Kuhusu Saccos ya Bumbuli, Kaboyoka alisema mbunge wake anafahamika, hivyo inashangaza ipewe fedha hizo kwa mwaka mmoja na kuhoji sifa zilizotumika kuzitoa wakati Saccoss zingine hazijapata.

Alisema ni vema ufanyike ukaguzi maalumu kwenye Saccos hiyo kwani fedha hizo ni mafao ya wafanyakazi ingawa pia inatia shaka katika utoaji, kwani awali Saccos hiyo ilipewa zaidi ya Sh bilioni moja na kwamba hesabu hazioneshi, kwamba fedha hizo zilirejeshwa, lakini ndani ya mwaka mmoja ikapewa fedha zingine.

NSSF ilitoa mikopo kwa Saccos tisa kwa kiasi kinachozidi asilimia 50 ya thamani ya mali za Saccos husika, kinyume na sera ya Shirika ya kukopesha na ziliomba kiasi ambacho hazikustahili.

Katika ripoti ya CAG mbali na Bumbuli, Saccos zingine zilizopewa fedha nyingi ni Korongo Amcos, UMMA, SBC, Hekima, Ukombozi, Uzinza, Harbour na Umoja.

Akijibu hoja hizo, Profesa Wangwe alisema Saccos zilizopewa fedha zaidi ya mara mbili kwa mwaka ikiwamo ya Bumbuli iliyopewa Sh bilioni 2.473 kwa mwaka 2014/15, wakati anaingia kwenye nafasi hiyo, aliliona hilo kama tatizo hivyo kuagiza kufanyike ukaguzi maalumu.

Alisema waliokuwa wanasimamia Saccos hizo walisimamiswa kazi tangu Bodi mpya ilipoingia na kwamba walisitisha kutoa mikopo ya aina yoyote katika Saccos zote nchini, hadi uongozi wa Shirika utakapoanzisha utaratibu mpya.

“Watu wote waliohusika na ubadhirifu wameshaondolewa ofisini, tulishituka kuona namna fedha hizo zilivyotolewa, si zote zilizofika kwa wahusika, zingine ziliishia kwenye mikono ya watu, tuliona ni vema ufanyike ukaguzi maalumu,” alisema Profesa Wangwe.
 
 

Thursday, October 27, 2016

Mchungaji Rwakatare Kuwatoa Wafungwa Wengiine 43 gerezani kwa Kuwalipia Faini Zao

SeeBait

Mchungaji  Kiongozi wa Kanisa la Assemblies of God (Mlima wa Moto), Getrude Rwakatare amesema ataendelea na mpango wake wa kuwanusuru wafungwa wanaotumikia adhabu magerezani kwa kuwalipia faini ili warejee uraiani.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, alisema katika awamu ya pili ameamua kuwalipia wafungwa 43 waliopo katika magereza ya Mkoa wa Dodoma.

“Kampeni hii ya kuwalipia faini kati ya Sh 50,000 hadi 200,000 wafungwa waliopo magerezani imetupa moyo na Watanzania wengi wameguswa na hata kutupongeza. Kutokana na hali hii kanisa letu sasa limefanya hivyo tena na safari hii tunaelekea mkoani Dodoma,” alisema.

Mchungaji Rwakatare alisema kesho watawatoa wafungwa hao mkoani Dodoma ambapo vigezo walivyoangalia ni wanawake wanaonyonyesha, wagonjwa na wazee.

“Nasi tunatimiza maandiko ya Mungu katika kufanya hivi na kuunga mkono juhudi za Mwenyekiti wa Parole, Augustino Mrema,” alisema Mchungaji Rwakatare.

Alisema kutokana na makosa mbalimbali ya faini waliohukumiwa nayo wafungwa hayo, kanisa lao limetoa Sh milioni 6.8 kwa ajili ya kulipia faini hizo.

Awali Rwakatare kupitia kanisa lake, aliwalipia wafungwa 78 katika magereza matatu ya Keko, Segerea na Ukonga ya jijini Dar  es Salaam na kuachiwa huru baada ya kulipa faini ya Sh milioni 25 zilizochangwa na waumini wa kanisa hilo.
 
 

Thursday, October 27, 2016

Maagizo 10 ya Makamba kwa uongozi wa mkoa wa Katavi baada ya kukamilisha ziara

SeeBait

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe January Makamba ameendelea na ziara yake katika Mkoa wa Katavi kwa kutembelea kijiji cha Kabege ambapo aliangalia mradi Mkubwa wa Umwagiliaji wa Mwamkulu katika Manispaa ya Mpanda ambao kwasasa umesitisha kutoa huduma zake kwa kukosekana kwa maji ya kutosha katika Mto Katuma.

Katika kikao cha Majumuisho ya Ziara yake ya siku mbili katika Mkoa wa Katavi, Waziri Makamba ameutaka uongozi wa Mkoa huo kudhibiti yafuatayo:

1. Ongezeko la watu na mifugo ambayo kwa kiasi kikubwa inachangia uharibifu wa mazingira.

2. Kusitisha uchepushaji kwa Mto Katuma ambapo taarifa ya Mkoa ilieleza kuna jumla yamabanio 40 ambayo yanatumiwa na watu kuchepusha maji kwa ajili ya manufaa yao binafsi.

3. Uchimbaji hatari wa Madini usiofuata taratibu

4. Kuhuisha sheria ndogo ndogo za mazingira katika ngazi mbalimbali za Serikali za mitaa

5. Kuanisha maeneo maalumu ambayo yatatangazwa katika Gazeti la Serikali kama mazingiranyeti ili kuyapa ulinzi zaidi

6. Kusimamia uondoshwaji wa wavamizi katika Vyanzo vya maji

7. Kufanyika kwa sensa ya mifugo ili kujua Mkoa una mifugo kiasi gani na kubuni namna boraya kuhumudimia mifugo hiyo bila kuathiri mazingira

8. Ameahidi kuaanda andiko maalumu la Mradi wa Ziwa Katuma

9. Mmiliki wa Jema Sitalike Project kutafutwa popote alipo, leseni yake ya madini isitishwe,apigwe faini na kurekebisha eneo alilokuwa akitumia awali kwa shughuli za uchenjuaji wadhahabu.

10. Waziri Makamba meagiza Watendaji kata na Vijiji kutotoa vibali vya uchimbaji wa madini bila kufuata utaratimu wa Wizara ya Nishati na Madini.

Aidha Waziri Makamba amewasili Katika Mkoa wa Kigoma na kutembelea kiwanda cha Nyanza Mines nakuwapongeza kwa kuzalisha chumvi kwa kutumia nishati ya jua ambapo awali kiwanda hicho kilifungiwa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kutokana na uharibifu wa Mazingira kwa kutumia magogo mengi mwaka 2015. Kiwanda hicho kwa sasa kinazalisha tani 20,000-25,000 ndani ya miezi mitatu.
 

Thursday, October 27, 2016

Kigogo wa Jeshi la Polisi Ashushwa cheo....Mwingine Atimuliwa

SeeBait



Mkuu wa jeshi la Polisi, IGP Ernest Mangu Jeshi la Polisi limemvua cheo mkuu wake wa kituo cha Himo (OCS), Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP), Zuhura Suleiman kwa tuhuma za kukutwa na gari la wizi aina ya Toyota Rav4. 
Pia, jeshi hilo limemfukuza kazi kwa fedheha (kwa kutolipwa haki zozote) ofisa wake mwingine wa cheo cha koplo, Federika Shirima ambaye naye anatuhumiwa kukutwa na magari mawili yaliyoibwa jijini Dar es Salaam. 
Hatua ya jeshi hilo dhidi ya askari wake imekuja siku chache baada ya kufichuka kwa tuhuma hizo ambazo zilionekana kulipaka matope. 
Alipohojiwa na wanahabari Jumatatu iliyopita kuhusu tuhuma za kukutwa na gari hilo lililoibwa pia Dar es Salaam, ASP Zuhura alikanusha na kusisitiza kuwa hazijui. 
“Hiyo taarifa (ya gari) mbona siijui. Hakuna taarifa kama hizo,” alikanusha taarifa hizo ambazo baadaye zilithibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa ambaye alikiri maofisa wake kukutwa na magari hayo, lakini akasema hawawezi kupewa adhabu kabla ya kuthibitika kuwa amefanya uhalifu.
“Makachero wetu wanashirikiana na kikosi kazi cha Dar es Salaam na watakapobainika hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao,” alisema. 
Taarifa zilizopatikana jana zilisema, ofisa mwenye cheo cha koplo alisomewa barua ya kufukuzwa kazi juzi jioni na muda huohuo na ASP Zuhura naye akasomewa barua ya uhamisho. 
“Kwa cheo cha ASP mamlaka yake ya nidhamu ni katibu mkuu kwa hiyo kilichofanyika ni kumuondoa kwenye wadhifa wa OCS akisubiri uamuzi mwingine kutoka juu,” kilidokeza chanzo chetu. 
ASP Zuhura alipotafutwa kwa simu jana ili kuzungumzia suala hilo hakupokea, lakini Koplo Federika alipopigiwa alipokea na kukana kufukuzwa kazi kisha kukata simu. 
Kamanda Mutafungwa alipopigiwa simu alitaka atumiwe ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) na alipotumiwa na kuulizwa kuhusu suala hilo, hakukanusha wala kuthibitisha zaidi ya kujibu atafutwe leo saa 5:00 asubuhi. 
Kukamatwa kwa maofisa hao kulitokana na kutajwa na mtandao wa wizi wa magari jijini Dar es Salaam uliokuwa mikononi mwa polisi, ambao walisafiri hadi Himo na kuyakamata. 
Akizungumza jana katika mkutano na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro alisema mtandao huo umekuwa ukipeleka magari ya wizi Arusha na Moshi. 
Credit: Mwananchi
 
 

Thursday, October 27, 2016

Aliyejifanya Usalama wa Taifa Ahukumiwa Miaka Miwili Jela

SeeBait

Mahakama  ya Wilaya ya Ilala imemhukumu Seleman Manoti, kifungo cha miaka miwili jela kwa kupatikana na hatia ya kujifanya usalama wa Taifa.

Hata hivyo, mahakama imetoa hukumu hiyo bila mshitakiwa kuwepo mahakamani kutokana na kuruka dhamana kesi hiyo ilipokuwa inasikilizwa.

Akitoa hukumu hiyo jana, Hakimu Mkazi, Flora Haule alisema kuwa upande wa mashitaka, ulileta mashahidi wanne kwa ajili ya kuthibitisha tuhuma hizo.

Alisema kutokana na ushahidi uliotolewa, mahakama imeridhishwa na ushahidi huo na kwamba mahakama inamtia hatiani mshitakiwa licha ya yeye kutokuwepo.

“Hati ya kumkamata mshitakiwa itolewe na adhabu hii itaanza kutumika pindi mshitakiwa atakapokamatwa kwani alitoroka akiwa na haki ya kusikilizwa,” alisema Hakimu Haule.

Wakili wa Serikali, Ester Kyara aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mshitakiwa iwe fundisho kwa wengine.

Inadaiwa kuwa Novemba 19, 2014 maeneo ya Kariakoo Msimbazi wilayani Ilala, mshitakiwa alijitambulisha kwa Issaya Odelo na Charles Odinga kuwa Ofisa Usalama wa Taifa, kitu ambacho alijua si kweli. 

Katika hatua nyingine, kondakta Ally Salum (23), mkazi wa Mwananyamala, amehukumiwa kifungo cha miaka mitano jela baada ya kupatikana na hatia ya kuiba daladala.

Mbali na mshitakiwa huyo, Exavery Kaunga (44) ambaye ni mlinzi na mkazi wa Kiwalani, Minazi Mirefu, aliachiwa baada ya ushahidi dhidi yake kuwa na shaka.

Akitoa hukumu hiyo jana katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Hakimu Mkazi Mwandamizi, Juma Hassan, alisema kuwa upande wa mashitaka ulileta mashahidi wanne kuthibitisha kosa hilo.

“Nimeridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka, nakutia hatiani mshitakiwa kama ulivyoshitakiwa kwa kutumikia kifungo cha miaka mitano jela,” alisema Hakimu Hassan.

Kabla ya kutolewa adhabu hiyo, Wakili wa Serikali, Grace Mwanga aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mshitakiwa ili iwe fundisho kwa wengine. Hata hivyo, mshitakiwa alipoulizwa ni kwa nini asipewe adhabu kali, hakujibu chochote na mahakama kutoa adhabu hiyo.

Washitakiwa hao walishitakiwa kwa makosa mawili ya kula njama kutenda kosa ambapo inadaiwa kati ya Julai 5, mwaka jana, washitakiwa walikula njama kutenda kosa.

Pia inadaiwa Julai 5,2015 pembezoni mwa barabara ya Nyerere katika Kituo cha Mafuta cha Victoria, washitakiwa waliiba gari lenye namba za usajili T 624 CSH aina ya Eicher mali ya Kampuni ya White Swan. 
 
 

Thursday, October 27, 2016

Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Alhamisi ya Octoba 27

SeeBait
HABARI ZA ALHAMISI HII HABARI ZA ALHAMISI HII Reviewed by RICH VOICE on Oktoba 27, 2016 Rating: 5

Hakuna maoni

Chapisho Lililoangaziwa

Thursday, September 15, 2016 Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Alhamisi Ya Septemba 15 ...