Treni Yanusurika Kuchomwa Moto na Wananchi....Vioo 30 vya Mabehewa Vyapasuliwa, 17 Watiwa Mbaroni
TRENI
ya abiria inayofanya safari zake kati ya Kituo Kikuu cha Reli na
maeneo ya Pugu Dar es Salaam maarufu kama ‘Treni ya Mwakyembe’ nusura
ichomwe moto juzi, baada ya wananchi kudai kuchoshwa na usumbufu wa
shirika hilo.
Wananchi
hao walitaka warudishiwe nauli zao kwa kile walichodai Shirika la
Reli Tanzania (TRL) limeshindwa kuwa na ratiba inayoeleweka.
Tukio
hilo lilitokea juzi saa 3:00 usiku eneo la Majumbasita, baada ya treni
hiyo kukaa kituoni hapo kwa muda mrefu bila kuambiwa kuambiwa chochote.
Hali
hiyo iliwafanya abiria kuvamia kituo kidogo cha mawasiliano kilichopo
eneo hilo wakitaka warejeshewe nauli zao vinginevyo wangekichoma moto
pamoja na mabehewa ya treni hiyo.
Mwandishi
aliwashuhudia abiria wakitaka kuingia ndani ya kituo hicho huku
wakiwalazimisha wafanyakazi waliokuwapo wawarudishie fedha zao za nauli.
Purukushani hiyo iliyodumu kwa takribani saa mbili ilimalizika kwa abiria hao kuvunja vioo vya mabahewa ya treni vipatavyo 30.
Wafanyakazi
kuona hivyo walijifungia ndani ya kituo hicho huku polisi waliokuwa
wakisindikiza treni hiyo wakitimua mbio kunusuru maisha yao.
Baadhi
ya abiria walisema tangu Ijumaa iliyopita wamekuwa wakipata
usumbufu kwa kukatishiwa tiketi huku treni ikichelewa na wakati
mwingine kutoonekana kabisa.
Walisema
jambo hilo limekuwa likiwasababishia hasara na kuwalazimu kutafuta
usafiri mwingine na kuchelewa kufika kwenye majukumu yao.
Kufuatia
kukithiri vitendo vya uharibifu wa miundombinu ya reli na treni
vinavyofanywa na baadhi ya wananchi, Kampuni ya Reli Tanzania (TRL)
kupitia kwa Mkurugenzi Mtendaji , Masanja Kadogosa imetoa onyo kwa wananchi kutofanya vitendo hivyo.
“Tukio
hili si mara ya kwanza kujitokeza, lilijitokeza tarehe 24, 26 na 28
mwezi wa 10 na Novemba 7 Katika matukio hayo kulitokea uharibifu wa
miundombonu na kujeruhi baadhi ya wafanyakazi wa TRL akiwemo Mustapha
Omary ambaye ameshonwa nyuzi 8 katika hospitali ya mnazi mmoja,” amesema.
Amesema
kutokana na uharibifu huo, watuhumiwa 17 wanashikiliwa na jeshi la
polisi na kwamba upepelezi ukikamilika watachukuliwa hatua za kisheria.
Kadogosa
amedai kuwa, wahusika wa fujo na uharibifu huo ni makondakta wa dalala
kwa lengo la kutisha wananchi kutoutumia usafiri wa treni.
“Kuna
watu wa daladala wanafikiri wataendelea kufanya fujo ili wananchi waone
kuwa usafiri wa treni si salama wapande magari yao, sisi hatulazimishi
wananchi kuutumia usafiri wetu ila kutokana na ubora wa huduma zetu
wanakuja wenyewe. Pia hatusitishi kutoa huduma kwa sababu ya fujo zao
sababu tutawatesa abiria wetu zaidi ya 21,000,”
Naibu
Kamishna wa Polisi na Kamanda wa Reli, Simon Chillery amesema jeshi la
polisi linaendelea kufanya uchunguzi ili kubaini wengine waliohusika.
Rais Barack Obama ampongeza Rais Mteule, Donald Trump na kumualika Ikulu kujadiliana juu makabidhiano ya ofisi.
Rais
Barack Obama wa Marekani amempongeza Rais Mteule wa taifa hilo, Donald
Trump na kumualika Ikulu kujadiliana juu makabidhiano ya ofisi.
Msajili wa vyama vya siasa Tanzania, avifutia usajili Vyama Vitatu
Msajili
wa Vyama vya Siasa nchini Tanzania Jaji Francis Mutungi ametangaza
kuvifutia usajili vyama vitatu baada ya kubainika kukiuka sheria ya
usajili wa vyama.
Vyama
hivyo ni pamoja na CHAUSTA kilichopata usajili wa kudumu tarehe 5
Novemba 2001, The African Progressive Party of Tanzania (
APPT-Maendeleo) kilichopata usajili wa kudumu terehe 4 Machi 2003 na
Chama cha Jahazi Asilia kilichopata usajili wa kudumu tarehe 17 Novemba
2004.
Jaji
Mutungi amesema kuwa mchakato wa kufuta usajili wa vyama hivyo
umetokana na zoezi la uhakiki wa utekelezaji wa masharti ya usajili na
matakwa mengine ya sheria ya vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu
lililofanyika kuanzia tarehe 26 Juni hadi 26 Julai 2016.
Amesema
katika zoezi hilo uhakiki ulibaini kuwa vyama hivyo vimepoteza sifa za
usajili wa kudumu kwa kukiuka masharti ya sheria ya vyama vya siasa, na
kwamba kila chama kilipewa ya nia ya msajili kufuta usajili wake, lakini
vikashindwa kutoa utetezi wa kuridhisha ili visifutiwe usajili.
Kufuatia
uamuzi huo, Msajili amewataka waliokuwa wanachama wote wa vyama hivyo
kutojiuhusisha na shughuli yoyote kwa majina ya vyama hivyo, na kwamba
kufanya hivyo ni kuvunja sheria, huku akiviasa vyama vingine kuendesha
shughuli zao kwa kuzingatia sheria.
Breaking News: Donald Trump Ndo Mshindi wa Kiti cha Urais wa Marekani
Mgombea
wa Chama cha Republican, Donald Trump ameshinda uchaguzi mkuu wa
Marekani baada ya kufikisha kura 276 huku Hillary Clinton akiwa na kura
218.
Hillary Clinton amempigia simu Rais Mteule wa Marekani, Donald Trump na kumpongeza kufuatia ushindia huo alioupata.
Akizungumza
na wafuasi wake baada ya kutangazwa mshindi, Trump amewataka raia wote
wa Marekani, waliomchagua na ambao hawakumchagua kuungana na kuanza
kuijenga nchi yao kwani muda wa kampeni na siasa za kugawanyika
umekwisha.

Rais Magufuli Ampongeza Donald Trump Kwa Kushinda Kiti cha Urais Wa Marekani
Leo November 9, 2016 Marekani imeweka historia nyingine baada Donald
Trump wa chama cha Republican kutangazwa mshindi wa kiti cha Urais, na
tayari ameanza kupokea pongezi kutoka kwa viongozi wa nchi mbalimbali
ikiwemo Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli.
Rais Magufuli ametoa pongezi zake kwa Rais Donald Trump kupitia ukurasa wake Twitter
Ratiba ya Mazishi ya Spika Mstaafu, Samwel John Sitta
Mwili
wa aliyekuwa spika wa bunge, Samuel Sitta unatarajia kuwasili nchini
siku ya Alhamis ukitokea nchini Ujerumani ambapo alipokuwa akipatiwa
matibabu.
Taarifa hiyo imetolewa na Gerald Mongela ambaye ni msemaji wa familia.
Amesema
mara baada ya mwili huo kuwasili nchini utapelekwa nyumbani kwa
marehemu Masaki jijini Dar es Salaam na siku ya Ijumaa shughuli za kuaga
zitafanyika katika viwanja vya Karimjee kisha kupelekwa bungeni mjini
Dodoma.
“Mwili
wa mpendwa wetu mheshimiwa Samuel Sitta utawasili na ndege ya Emirates
siku ya Alhamis saa tisa na nusu alasiri na baada ya hapo mwili
tutauleta hapa nyumbani kwaajili ya kukaa nao na kupumzika kusubiri
ratiba ya Ijumaa,”alisema Mongela.
Mazishi ya Marehemu Samwel John Sitta yatafanyika siku ya Jumamosi Urambo mkoani Tabora.
Serikali: Ukosefu wa ajira kwa vijana umepungua
Serikali
ya Tanzania imesema kwamba kulingana na takwimu inaonesha kuwa ukosefu
wa ajira kwa vijana nchini Tanzania umepungua kwa asilimia mbili,
kutoka asilimia 13.7 mwaka 2012 mpaka asilimia 11.7 mwaka huu.
Akizungumza jana
bungeni, mjini Dodoma wakati wa kipindi cha maswali na majibu Naibu
Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira na Walemavu Mhe.
Anthony Mavunde, alisema
licha ya kupungua huko kwa ukosefu wa ajira, serikali imeweka mipango
ya kuwawezesha vijana kuwa na wigo mpana wa ajira nchini.
Mhe. Mavunde alisema
kuwa kwa takwimu hizo Tanzania ni nchi inayoongoza kwa kutoa ajira kwa
vijana wengi zaidi kushinda baadhi ya nchi za Afrika Mashariki ikiwemo
Kenya na Uganda.
TRA Yakusanya Shilingi Trilioni 1.15 Mwezi Oktoba
Na Ally Daud-MAELEZO.
MAMLAKA
ya Mapato Tanzania (TRA) imefanikia kukusanya shilingi trilioni 1.15
kwa mwezi Oktoba ikiwa ni kukamilisha malengo waliyojiwekea katika
ukusanyaji wa mapato.
Hayo
yamesemwa na Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa kodi Bw. Richard
Kayombo wakati wa mkutano na waandishi wa habari leo jijini Dar es
salaam kuhusu hali ya makusanyo na zoezi la uhakiki wa namba za
utambulisho wa mlipa kodi (TIN)linaloendelea hivi sasa.
“Tumefanikiwa
kukusanya shilingi Trilioni 1.15 kwa mwezi Oktoba mwaka huu ikiwa ni
kufanikisha malengo ya ukusanyaji kodi nchini ili kukuza uchumi wa nchi
pamoja kusaidia Serikali kuendeleza huduma za jamii nchini” alisema Bw. Kayombo.
Aidha
Bw. Kayombo amesema kuwa mapato hayo yametokana na mikakati thabiti
iliyowekwa na mamlaka hiyo katika ukusanyaji kodi hapa nchini ili kuweza
kusaidia ongezeko la pato la Taifa .
Katika
hatua nyingine TRA imefanikiwa kushinda kesi 9 kati ya 10 zilizokuwa
zikiendelea katika mahakama mbalimbali nchini dhidi ya walipa kodi wake
na kufanikiwa kupata kiasi cha takribani Bilioni 16.9 .
“Tumefanikiwa
kushinda kesi 9 kati ya 10 ambazo zilifikishwa mahakamani dhidi ya
walipa kodi na kupata kiasi cha shilingi bilioni 16.9 hivyo kufanya
juhudi zetu za kukusanya mapato mengi zaidi” aliongeza Bw. Kayombo.
Mbali
na hayo Bw. Kayombo amesema kuwa zoezi la uhakiki wa namba za
utambulisho wa mlipa kodi ambalo limeanza hivi karibuni linaendelea na
litafikia tamati Novemba 30 mwaka huu kwa mkoa Dar es salaam hivyo
wananchi kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya uhakiki huo.
Aidha
Bw. Kayombo ameongeza kuwa kila mwenye namba ya utambulisho wa mlipa
kodi anatakiwa akahakiki kwa ajili ya kupata taarifa sahihi za mlipa
kodi ili kuepuka kufutwa kwa namba yake ya utambulisho baada ya zoezi
hilo kumalizika kwa mkoa husika.
HABARI ZA KIMATAIFAA
Habari
| 09.11.2016 | 16:16
Rais Barack Obama wa Marekani amemwalika ikulu hapo kesho alkhamisi
mshindi wa uchaguzi wa rais Donald Trump. Msemaji wa ikulu ya
Marekani,Josh Earnest amesema rais Obama anapanga kumueleza Trump kuhusu
kipindi cha mpito kilichoandaliwa na washirika wake.Tajiri huyo
asiyekuwa na maarifa yoyote ya kisiasa ameshinda kwa mshangao wa
wengi,uchaguzi wa rais na ataingia ikulu ya White House january 20 kama
rais wa 45 wa Marekani. Katika hotuba yake ya ushindi mara baada ya
matokeo ya uchaguzi kutangazwa,Trump amesema atakuwa rais wa kila
mmarekani. Kuhusu siasa ya nje,ameahidi kushirikiana na mataifa yote
yatakayokuwa tayari kufanya hivyo. Chama cha Trump,Republican
kinashikilia pia wingi wa viti katika mabaraza yote mawili ya bunge la
Marekani-Congress
Kansela Angela Merkel amempongeza rais mteule wa Marekani Donald
Trump.Akizungumza mjini Berlin kansela Angela Merkel amekumbusha
uhusiano wa dhati kati ya nchi hizi mbili na kusema:"Ujerumani na
Marekani zinashikamana chini ya misingi ya Demokrasia,uhuru,kuheshimu
haki na hadhi ya binaadamu bila ya kujali asili yake,rangi yake ya
ngozi,dini,jinsia wala mwelekeo wake kijinsia au kisiasa. Natangaza
utayarifu wa kushirikiana na Trump chini ya misingi hiyo ya
maadili."Wanasiasa nchini Ujerumani wamepigwa na mshangao kutokana na
ushindi wa Donald Trump. Mambo hayatakuwa rahisi,yatakuwa magumu zaidi
amesema waziri wa mambo ya nchi za nje Frank-Walter Steinemeier huku
waziri wa ulinzi Ursula von der Leyen akiutaja ushindi wa Donald trump
kuwa ni mshituko mkubwa.
Mwenyekiti wa baraza la Ulaya,Donald Tusk na mwenzake wa halmashauri
kuu ya Umoja wa Ulaya,Jean-Claude Juncker wanapanga kuandaa haraka
iwezekanavyo mkutano wa kilele pamoja na rais mteule wa Marekani Donald
Trump. Katika risala yao ya pongezi,viongozi hao wa Umoja wa ulaya
wamemwalika Trump aitembelee Ulaya."Wakati huu ni muhimu kuliko wakati
wowote ule mwengine kuimarisha uhusiano miongoni mwa nchi zinazopakana
na bahari ya Atlantik,wamesema katika risala yao ya pongezi,wakizingatia
masuala kuhusiana na mabadiliko ya tabia nchi,mapambano dhidi ya
ugaidi,wakimbizi na mzozo wa Ukraine. Mkutano wa kilele kati ya Umoja wa
ulaya na Marekani utafungua njia ya kusawazisha mambo kwa kipindi cha
miaka minne inayokuja. Nae waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani
Frank-Walter Steinmeier amependekeza uitishwe mkutano wa mawaziri wa
nchi za nje wa nchi za Umoja wa Ulaya na Marekani. Mkutano huo ungepaswa
kuitishwa jumamosi ijayo mjini Luxemburg,siku moja kabla ya kikao cha
kawaida cha mawaziri wa nchi 28 wanachama wa Umoja wa Ulaya.Waziri mkuu
wa Uingereza Theresa May anasema nchi yake na Marekani ni washirika
wakubwa wa biashara,usalama na ulinzi na hali hiyo haitobadilika. Na
waziri mkuu wa Italy pia,Matteo Renzi amempongeza Trump na kusema ana
hakika uhusiano wa kirafiki kati ya Italy na Marekani utaendelea kuwa
madhubuti.
Maandamano dhidi ya Trump yameripotiwa karibu na pwani ya
California,baada ya mgombea wa chama cha Republican kutangazwa mshindi
wa uchaguzi wa rais-Habari hizo zimetangazwa na maripota wa shirika la
habari la Reuters na wa vyombo vyengine vya habari vya eneo hilo.
Waandamanaji wametia moto sanamu la Trump,wamevunja maduka na madirisha
na kutia moto taka taka na mipira ya magari katika eneo la
Oakland,katika pwani ya San Franasisco. Masafa machache kutoka
hapo,katika chuo kikuu cha California,wanafunzi wa Berkley pia
waliandamana katika uwanja wa chuo kikuu. Maandamano yameripotiwa pia
katika eneo jengine la chuo kikuu cha California-Davis ambako wanafunzi
waliweka vizuwizi majiani,na kuongozana huku wakiimba nyimbo dhidi ya
Donald Trump. Mwanaharakati mmoja aligongwa na gari huko Oakland
alipokuwa anaweka vizuwizi katika njia kuu.
Hakuna maoni