SATURDAY 10/09/2016

HABARI ZA KIMATAIFA


Marekani na Urusi zafikia makubaliano ya kusitisha mapigano Syria
Marekani na Urusi hii leo zimefikia makubaliano ya kusitisha mapigano nchini Syria yatakayoanza kutekelezwa mapema wiki ijayo, hatua ambayo itaenda sambamba na ushirikiano wa pamoja kijeshi kati ya mataifa hayo mawili katika kukabiliana na makundi ya itikadi kali ya Dola la Kiisilamu IS na mtandao wa kigaidi wa Al-Qaeda. Akizungumza katika kikao cha pamoja na waandishi wa habari kilichohudhuriwa pia na Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov, Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani John Kerry amesema mpango huo utasaidia kupunguza mgogoro huo wa Syria katika kuelekea kipindi cha mpito cha mchakato wa kutafuta suluhu ya kumaliza mgogoro huo uliodumu kwa muda wa miaka mitano sasa. Amesema iwapo mpango huo utaafikiwa na pande zote zinazohusika ikiwa ni pamoja na serikali ya Syria inayoungwa mkono na Urusi na makundi ya waasi nchini humo yanayoungwa mkono na Marekani, basi itakua ni hatua muhimu katika kuelekea kutafuta ufumbuzi wa mgogoro huo. Kerry amesema hatua hiyo ya usitishaji mapigano itakayoanza Jumatatu itasadifiana na sherehe za dini ya Kiisilamu za Eid al- Haji.
.............
Uturuki yataka kutengwa maeneo salama nchini Syria
Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Uturuki Mevlut Cavusoglu amesema kuna ulazima wa kutengwa  maeneo salama nchini Syria hatua itakayosaidia   wakimbizi kurejea kaskazini mwa nchi hiyo kufuatia majeshi ya Uturuki kufanikiwa kulirejesha nyuma kundi la wanamgambo wenye itikadi kali la Dola la Kiisilamu.  Akizungumza hapo jana mjini Ankara  katika kikao na  waandishi wa habari ambacho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya kujihami ya NATO Jens Stoltenberg, Cavusoglu amesema ili watu waweze kurejea katika makazi yao, lazima hatua hiyo iende sambamba na kuzuia mashambulizi ya angani. Alisema hilo si jukumu la NATO pekee  na kusisitiza kuwa mchango wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa unahitajika katika kufanikisha suala hilo. Kwa upande wake Katibu Mkuu wa NATO Jens Stoltenberg alipongeza juhudi za Uturuki katika kupambana na kundi la itikadi kali la Dola la Kiisilamu pamoja na makundi mengine ya kigaidi katika ukanda huo.
,,,,,,,,,,,,,,,
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuichukulia hatua Korea Kaskazini
Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa hapo jana limekubaliana kuanza mchakato wa kuchukua hatua zinazolenga vikwazo vipya dhidi ya Korea Kaskazini kufuatia nchi hiyo kufanya jaribio la tano la silaha za nyukilia ambalo limeshutumiwa na jumuiya ya kimataifa. Kwa mujibu wa balozi wa New Zealand kwenye Umoja wa Mataifa Gerard van Bohemen  ambaye kwa sasa anashikilia urais wa kupokezana wa baraza  la usalama, baraza hilo  litaanza mchakato wa kuchukua hatua za  haraka kwa kuzingatia ibara ya 41 ya azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa ajili ya kuiwekea vikwazo vipya Korea Kaskazini.  Korea Kusini, Marekani , Japan, Urusi na China zote zimelaani jaribio hilo. Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amelitaka baraza hilo kuungana na kuchukua hatua za haraka ambapo pia  amesema anajutia kushindwa kutoa mchango wa kutosha katika kutatua migogoro tofauti kama alivyotarajia. Korea Kaskazini tayari imekumbana na vikwazo mara tano vya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa tangu ilipoanza majaribio yake ya silaha za nyukilia mnamo mwaka 2006.
............



Bunge la Marekani lapitisha mswada kuhusu mashambulizi ya Septemba 11
Bunge la Marekani limeidhinisha muswada ambao utazipa nguvu familia ambazo ni wahanga wa mashambulizi  ya kigaidi ya Septemba 11 nchini Marekani kuishitaki serikali ya Saudi Arabia kutokana na kile kinachodaiwa  kufadhili ugaidi nchini Marekani.  Hatua hiyo inakuja mnamo wakati Marekani ikikaribia kuadhimisha kumbukumbu ya miaka 15 ya mashambulizi ya kigaidi yaliyofanyika mwaka 2001 nchini humo. Hata hivyo Rais Barack Obama ameapa kutosaini kuidhinisha muswada huo akisema unakiuka haki za msingi za mamlaka ya nchi iliyokusudiwa na muswada huo. Kwa upande wake Saudi Arabia imetishia kuondoa mabilioni yake ya dola katika uchumi wa Marekani endapo muswada huo utaidhinishwa kuwa sheria. Mashambulizi hayo ya Septemba 11, 2001 yaliwaua kiasi ya watu 3,000 wengi wao wakiwa raia wa Marekani
..................
Watu 40 waua katika shambulizi la bomu mjini Baghdad
Kiasi ya watu 40 wameuawa baada ya bomu lililokuwa katika gari kuripuka mjini Baghdad hapo jana . Zaidi ya watu 60 walijeruhiwa katika tukio hilo baada ya gari lililokuwa limejazwa vilipuzi kuripuka karibu na jengo lenye maduka mjini Baghdad.  Hakukuwa na taarifa za awali kuhusiana na waliohusika na shambulizi hilo ingawa mashambulizi mengi katika mji wa Baghdad yamekuwa yakihusishwa na kundi la wanamgambo wenye itikadi kali la Dola la Kiisilamu IS. Mashambulizi hayo ya IS  mara nyingi yamekuwa yakilenga maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu kama vile masoko na migahawa iliyoko katika maeneo ya washia  nchini humo

 

 

LEO NI DABI YA JIJI LA MANCHESTER – MAN UNITED v MAN CITY NDANI YA OLD TRAFFORD!

>>MOURINHO, GUARDIOLA ‘WAPOZA UHASAMA’!
LIGI KUU ENGLAND
Ratiba:
**Saa za Bongo
Jumamosi Septemba 10
1430 Man United v Man City                
1700 Arsenal v Southampton                
1700 Bournemouth v West Brom           
1700 Burnley v Hull          
1700 Middlesbrough v Crystal Palace               
1700 Stoke v Tottenham             
1700 West Ham v Watford          
1930 Liverpool v Leicester 
++++++++++++++++++++++++++
DABI-MANCHESTER-SEP10LEO Mchana Jiji la Manchester huko England litazizima kwa Mechi kubwa kabisa ya Dabi ya Jiji hilo kati ya Mahasimu wakubwa kabisa Manchester United na Manchester Mechi ambayo itachezwa Old Trafford ikiwa ni ya Ligi Kuu England, EPL.
Mechi hii imeongezwa utamu hasa kwa vile safari hii Timu hizi zinaongozwa na Mameneja waliokuwa na ‘uadui’ tangu wakiwa huko Spain wakiongoza Wapinzani wakubwa huko Real Madrid, ikiwa na Jose Mourinho, na FC Barcelona, wakiwa na Pep Guardiola.
Sasa Mourinho yupo Man United na Guardiola yupo Man City na Leo zinatinga Uwanjani zikiwa zote zimeshashinda Mechi zao zote 3 za kwanza za EPL Msimu huu.
Kila Timu imesheheni Mastaa wakubwa lakini City hii Leo inaingia ikiwa pungufu kwa kumkosa Straika wao mkubwa Sergio Aguero ambae Leo anaanza Kifungo chake cha Mechi 3 baada ya kupatikana na hatia ya kumpiga kiwiko Beki wa West Ham Winston Reid katika Mechi yao ya EPL iliyopita.
++++++++++++++++++++++++++
JE WAJUA?
-Kwa Misimu 7 kati ya 10 iliyopita, Bingwa wa Ligi Kuu England amekuwa ama Man United au Man City.
-Katika Dabi za Manchester 171, Man United wameshinda 71, Man City 49, Sare 51.
DAIMA: www.sokaintanzania.com
+++++++++++++++++++++++++++
Msimu huu, Klabu hizi mbili zimenunua Wachezaji kadhaa kwa Bei mbaya wakati Man United ilipomsaini tena Paul Pogba kutoka Juventus kwa Dau la Rekodi ya Dunia la Pauni Milioni 89 na Man City kumnunua Beki John Stones kutoka Everton kwa Pauni Milioni 47.5 ikiwa ni Rekodi kwa Beki.
Hapo jana, Mameneja wa Man United na Man City waliongea na Wanahabari na wote kugusia kinachodaiwa huo ‘uhasama’ kati yao na wote kupoza hilo.
Meneja wa City, Guardiola, alidokeza kuwa ‘uhasama’ wake na Meneja wa Man United Jose Mourinho umebuniwa na Vyombo vya Habari.
Ameeleza: “Hatuwezi kudhibiti hilo. Nimesema mara nyingi, namheshimu sana Mourinho. Daima najaribu kujifunza toka kwa wenzangu na hilo pia ni kwa Mourinho.”
Aliongeza: “Alikuwa Kocha wangu, Kocha Msaidizi na Sir Bobby Robson. Ni kweli kipindi cha mwisho huko Barcelona na Real Madrid haikuwa rahisi kwetu sisi lakini tumekutana Wiki 2 au 3 zilizopita kwenye Mkutano wa Mameneja wa Ligi Kuu England.”
“Ni wazi nitakubali kunywa nae Glasi ya Mvinyo baada ya Gemu kama akinikaribisha!
Nae Mourinho ameeleza: “Najua nini ni Dabi. Nimezichezea kila sehemu na nataka niwe mtulivu. Kama tukitakata kushinda lazima tuwe juu. Wao wana Meneja mzuri sana, Siku zote wamekuwa na Wachezaji wazuri sana na wamenunua wengine. Wao ni wapigania Ubingwa na lazima uwaheshimu!”
Kwenye Mechi yao iliyopita Msimu uliopita Mwezi Machi 2016, Man United iliifunga Man City 1-0 huko Etihad kwa Bao la Marcus Rashford.
VIKOSI VINATARAJIWA KUWA:
MAN UNITED [Mfumo 4-2-3-1]:
-De Gea
-Valencia, Bailly, Blind, Shaw
-Pogba, Fellaini
-Mata, Rooney, Martial
-Ibrahimovic
MAN CITY [Mfumo 4-3-3]:
-Bravo
-Sagna, Kolarov, Stones, Clichy
-Silva, Fernando, Fernandinho
-Nolito, Sterling, De Bruyne
REFA: Mark Clattenburg
LIGI KUU ENGLAND
Ratiba:
**Saa za Bongo
Jumapili Septemba 11
1800 Swansea v Chelsea   
Jumatatu Septemba 12
2200 Sunderland v Everton 

 

JOE HART KUCHEZA MECHI YAKE YA KWANZA NA TORINO YA ITALY


HARTKIPA wa England Joe Hart anatarajiwa kucheza Mechi yake ya kwanza huko Italy akiwa na Klabu yake ya Mkopo Torino hapo Jumapili wakiivaa Atalanta kwenye Ligi Serie A.
Lakini Mechi hii itakuwa ngumu kwa Hart kwani Torino wana wakati mgumu baada ya Wachezaji wao muhimu kuumia.
Baada kupiga Hetitriki wakati Torino ikiitwanga Boligna 5-1 Straika wao Andrea Belotti ameumia na ataikosa hii Mechi pamoja na Straika wao mwingine kutoka Venezuela Josef Martinez ambae aliumia kwenye Mechi ya Nchi yake ilipotoka 2-2 na Argentina hivi Juzi kwenye Mechi za Kanda ya Marekani ya Kusini kuwania nafasi kwenye Fainali za Kombe la Dunia za Mwaka 2018 huko Russia.
Kwenye Mechi nyingine za Serie A Wikiendi hii, Mabingwa Watetezi Juventus, ambao Wiki ihayo watacheza na Sevilla kwenye Mechi yao ya kwanza ya Kundi lao la UEFA CHAMPIONZ LIGI, watacheza na Sassuolo.
SERIE A
Ratiba
Jumamosi Septemba 10
Juventus FC v US Sassuolo Calcio
U.S. Citta di Palermo v SSC Napoli
Jumapili Septemba 11
Bologna FC v Cagliari Calcio
AC Milan v Udinese Calcio
Atalanta v Torino FC
AC Chievo Verona v SS Lazio
AS Roma v UC Sampdoria
Genoa CFC v ACF Fiorentina
Pescara v Internazionale Milano
Jumatatu Septemba 12
Empoli v Crotone

 

 MICHEZOOOO

 VPL: LEO MABINGWA YANGA KUIBOMOA MAJIMAJI? MTANANGE SOKOINE MBEYA FC v AZAM FC! SIMBA JUMAPILI NA MTIBWA!


LIGI KUU VODACOM
Jumamosi Septemba 10
Mwadui FC v Stand United
Mbeya City v Azam FC
Ndanda FC v Kagera Sugar
Yanga v Majimaji FC
Ruvu Shooting v JKT Ruvu
++++++++++++++++++++++
VPL-2016-17-LOGO-1LEO Ligi Kuu ya Vodacom, VPL, ina Mechi 5 na Mabingwa Watetezi Yanga wapo Uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam kucheza na Majimaji FC.
Yanga walianza utetezi wa Taji lao kwa kuifunga African Lyon 3-0 na Juzi huko Nangwanda walibanwa na kutoka 0-0 na Ndanda FC nah ii Leo watasaka ushindi kwa udi na uvumba ili kurudi kwenye Reli.
Kocha wa Yanga Hans van Pluijm amesema wao Leo wamejitayarisha ili kushinda ili wakae sawa kwenye Ligi.
Baada ya Mechi 2, Yanga wana Pointi 4 wakiwa nafasi ya 7 kwenye Msimamo wa VPL ambayo inaongozwa na Azam FC wenye Pointi 7 kwa Mechi 3 na ambao Leo wako huko Sokoine Jijini Mbeya kuwavaa Mbeya City ambao wamecheza Mechi 3 na wana Pointi 7 pia.
Wakati Kocha kutoka Spain wa Azam FC, Zeben Hernandez, akikiri Mechi hii ni ngumu kwao, Kocha kutoka Zambia wa Mbeya City, Kinnah Phiri, amebainisha kuijua Azam FC baada ya Juzi kuiona ikicheza na Tanzania Prisons.
Nao Simba, ambao wana Pointi 7 kwa Mechi 3 na wako Nafasi ya 3, watacheza Jumapili Uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam dhidi ya Mtibwa Sugar ambao wamecheza Mechi 3, wana Pointi 6 na wapo Nafasi 4.
MSIMAMO:
NA
TIMU
P
W
D
L
F
A
GD
PTS
1
Azam FC
3
2
1
0
5
1
4
7
2
Mbeya City
3
2
1
0
5
1
4
7
3
Simba
3
2
1
0
5
2
3
7
4
Mtibwa Sugar
3
2
0
1
4
3
1
6
5
Kagera Sugar
3
1
2
0
1
0
1
5
6
Stand United
3
1
2
0
1
0
1
5
7
Yanga
2
1
1
0
3
0
3
4
8
Ruvu Shooting
3
1
1
1
3
3
0
4
9
Tanzania Prisons
3
1
1
1
2
2
0
4
10
Mwadui FC
3
1
0
2
1
2
-1
3
11
Toto Africans
3
1
0
2
1
2
-1
3
12
JKT Ruvu
2
0
2
0
0
0
0
2
13
African Lyon
3
0
2
1
1
4
-3
2
14
Ndanda
3
0
1
2
2
5
-3
1
15
Mbao FC
3
0
1
2
1
5
-4
1
16
Majimaji
3
0
0
3
1
6
-5
0
LIGI KUU VODACOM
Jumapili Septemba 11
Simba v Mtibwa Sugar
Tanzania Prisons v Toto Africans
Jumapili Septemba 12
African Lyon v Mbao FC

 

 

Saturday, September 10, 2016

Tamko La Waziri Wa Afya, Maendeleo Ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto Kuhusu Watoto Waliomaliza Elimu Ya Msingi Lililotolewa Tarehe 09/09/2016

SeeBait

TAMKO LA MHESHIMIWA UMMY MWALIMU (MB) WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO KUHUSU WATOTO WALIOMALIZA ELIMU YA MSINGI LILILOTOLEWA TAREHE 09/09/2016

Ndugu Wanahabari, Nitumie fursa hii kupitia kwenu kuongea na watoto wa Tanzania, wazazi / walezi na jamii kwa ujumla katika kipindi hiki muhimu ambacho watoto wetu wamemaliza Elimu ya Msingi.  Kwa niaba yangu na kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza watoto wote waliomaliza mtihani wa Taifa wa kuhitimu Elimu ya Msingi mwaka huu, Hongereni sana!. Ni jambo la ufahari kwetu sisi wote kama wazazi/ walezi na Taifa kwa ujumla kwani hii ni fursa adhimu kwa ustawi na maendeleo ya mtoto na ni moja ya njia ya kutimizwa kwa haki ya msingi ya mtoto ya kuendelezwa ambayo inamjengea mtoto msingi imara wa maisha yake ya baadae. Pongezi zangu nyingi kwa watoto wote wa kike na wa kiume walioweza kufikia hatua hii muhimu kwa maendeleo na ustawi wao.

Ndugu Wanahabari, Takwimu zinaonyesha kuwa, wanafunzi 795,761 (wavulana 372,883 sawa na asilimia 46.86 na wasichana 422,878 sawa na asilimia 53.14) wamesajiliwa kufanya mtihani wa darasa la saba mwaka huu. Hivyo ningependa kutumia fursa hii kuwaasa watoto waliomaliza darasa la saba kutojihusisha na tabia au vitendo vyovyote vinavyo hatarisha afya, usalama na maendeleo yao, kama vile kujihusisha kwenye masuala ya ngono, matumizi ya madawa ya kulevya na vileo katika kipindi hiki cha kusubiri matokeo ya mitihani yao.

 Watoto wetu wa Kike na Kiume wajitambue, na wajue kuwa wao ni hazina ya pekee katika maendeleo ya nchi yetu. Kipindi hiki wakitumie vizuri kwa kuwa waadilifu, waaminifu, wenye bidii na kuzingatia kanuni za nidhamu na tabia njema huku wakijiandaa kwa ajili ya kuendelea na elimu ya Sekondari. Tukumbuke kuwa Serikali imekusudia kumpa kila mtoto nafasi ya kupata elimu ya Sekondari. Msingi tayari umeshawekwa na Rais wa Awamu ya tano, Mheshimiwa John Pombe Magufuli wa kutoa Elimu ya Sekondari bure. Hivyo tusingefurahi mmojawapo kati ya watoto hawa waliomaliza elimu ya msingi jana akaikosa nafasi hii kwa sababu zinazoweza kuzuilika. Nawaasa watoto wote kutumia kipindi hiki kwa kukataa kurubuniwa, kushawishiwa na kujiingiza katika mambo yenye kuhatarisha afya, usalama na maendeleo yao.

Ninawataka Wazazi wenzangu, Walezi na jamii kwa ujumla:-
Kutowaozesha watoto wote wa kike waliohitimu darasa la saba mwaka huu wakati wa kipindi hiki cha kusubiria matokeo yao, iwe ni kwa sababu yoyote ile au kwa lengo la kujipatia mali kwa njia ya mahari. Kila Mzazi/Mlezi anapaswa kutambua umuhimu wa mtoto wake kuendelea kielimu, na kukua kimwili na kiakili kabla ya kuingia katika ndoa. Ieleweke kuwa Elimu ya watoto wa kike ni moja ya njia bora za kupunguza umaskini katika mataifa yanayostawi. Kila mwaka wa elimu kwa mwanamke utaongeza mapato yake ya baadae kwa asilimia 15, ikilinganishwa na asilimia 11 kwa wanaume. Aidha, Kila mwaka wa mtoto wa kike kuwa shule humuepusha na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) mara 7.

Pia, uzoefu unaonyesha kuwa, kila mwaka wa kuelimika humsaidia msichana kufanya maamuzi bora yake na ya familia yake. Benki ya Dunia ilibainisha ya kwamba kila mwaka wa elimu huzuia vifo 2 vya uzazi katika wanawake 1000 kila mwaka!. Kwa hiyo kumpa mtoto wa kike fursa ya elimu inamsaidia sio yeye tu kukua kiakili na kimwili lakini pia inamnusuru na ndoa na mimba za utotoni na kuchangia maendeleo yake, ya familia yake na jamii kwa ujumla. Ni vyema jamii hasa wazazi na walezi wafahamu kuwa ndoa kwa wasichana sio njia muafaka ya kutatua changamoto za kifedha za wazazi/walezi. Bali elimu ndio njia bora ya kutatua changamoto hizo.

Kuwalinda watoto wote wa kike na wa kiume waliohitimu darasa la saba mwaka huu dhidi ya vitendo vyote vya Ukatili, hasa kwa watoto wa kike kupewa mimba au kuwahusisha katika mahusiano ya kimapenzi. Kwa mujibu wa Sheria ya makosa ya kujamiiana ya mwaka 1998 ambayo imefanyiwa marekebisho na kuhuishwa kwenye Makosa ya Jinai (Penal Code Cap 16)  inaelekeza kuwa ni kosa la jinai  kwa mtu yoyote kumlaghai mtoto wa chini ya miaka  18 kwa kumpa mimba au kufanya nae mapenzi.

 Kifungu cha 130 (e) cha Sheria hii kinaeleza wazi kuwa “Ni kosa kwa mtu wa jinsia ya kiume kumbaka msichana au mwanamke; kwa ridhaa au bila ya ridhaa akiwa chini ya umri wa miaka kumi na nane. Mtu yeyote atakayetenda kosa la kubaka atawajibika kwa adhabu ya kifungo cha maisha au kifungo kisichopungua miaka thelathini. Aidha, Sheria ya Mtoto Namba 21 ya mwaka 2009 Kifungu cha 83 kinaelekeza kuwa ni kosa kumuhusisha mtoto katika kazi, biashara au mahusiano yoyote yenye mlengo wa kingono iwe ni kwa malipo au bila malipo.

Mkono wa Serikali ni mrefu. Tutahakikisha tunawakamata na kuwafikisha Mahakamani wale wote watakao kwenda kinyume na sheria hizi.

Aidha, natoa Rai kwa wananchi wote kuendelea kutoa taarifa kwa mamlaka husika za Serikali za Mtaa, Kijiji, Kata, Wilaya na hata katika Madawati ya Jinsia na Watoto yaliyopo Polisi, pale watakapobaini mzazi au mlezi au taasisi anaenda kinyume na jitihada za serikali za kumuendeleza mtoto kielimu hasa katika kudhibiti ndoa za watoto waliomaliza Elimu ya Msingi hususan katika kipindi hiki cha kusubiri matokeo yao.

Vunja ukimya toa taarifa kwa maendeleo ya watoto wetu.
Nawatakia kila la kheri watoto wote wa Tanzania katika kipindi hiki cha kusubiri matokeo yao ya mtihani wa Elimu ya msingi.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu wabariki watoto wa Tanzania.

Imetolewa na:-
UMMY A. MWALIMU (MB)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA,
WAZEE NA WATOTO
DODOMA
09/09/2016

 

 

 

Saturday, September 10, 2016

Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Jumamosi Ya Septemba 10

SeeBait
Reviewed by RICH VOICE on Septemba 10, 2016 Rating: 5

Hakuna maoni

Chapisho Lililoangaziwa

Thursday, September 15, 2016 Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Alhamisi Ya Septemba 15 ...