habari za jumamosi ya leooo

 Saturday, September 24, 2016

Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Jumamosi ya Septemba 24

SeeBait

 

 

 

Saturday, September 24, 2016

Majaliwa Aipa Siku 10 Taasisi Ya Hifadhi Ya Bahari Kulipa Deni La Sh. Milioni 100

SeeBait
WAZIRI MKUU  Mhe. Kassim Majaliwa ametoa muda wa siku 10 kwa Taasisi ya Hifadhi ya Bahari na Maeneo Tengefu kulipa deni la sh. milioni 100 inayodaiwa na Halmashauri ya wilaya ya Mafia.
 
Deni hilo linatokana na malimbikizo ya miaka mitatu ya maduhuri yatokanayo na makusanyo yanayofanywa na taasisi hiyo katika maeneo ya hifadhi ya bahari wilayani humo.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo Ijumaa, Septemba 23, 2016 wakati akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya wilaya hiyo katika ukumbi Caltas akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi siku mbili.
 
“Waandikieni barua na muitume leo hii kwa njia ya mtandao (email) kuwajulisha kuwa wanatakiwa kulipa deni hilo ndani ya siku 10. Hakikisheni wanalipa deni hili ili Halmashauri iweze kufanya kazi zake vizuri,” amesema.
 
Waziri Mkuu amesema Serikali inataka kuona Halmashauri hiyo ikinufaika kutokana na vyanzo vyake vya mapato, hivyo haitakuwa tayari kuona ikihangaika.
 
Mbali na agizo hilo, Waziri Mkuun amesema atafuatilia kuona wajibu wa taasisi hiyo na mipaka yao ikiwa ni pamoja na kujua mapato yatokanayo na shughuli hizo katika maeneo ya hifadhi.
 
Awali mkuu wa wilaya ya Mafia Shaib Nnunduma alisema kuwa miongoni mwa changamoto zinazoikabili wilaya hiyo ni kutolipwa kwa wakati fedha za maduhuri yatokanayo na makusanyo yanayofanywa na Taasisi ya Hifadhi ya Bahari.
 
Mkuu huyo wa wilaya ameiomba Serikali kuangalia upya majukumu ya taasisi hiyo na nafasi ya halmashauri katika kuendesha shughuli za uwekezaji pamoja na kupata mapato yatokanayo na shughuli hizo katika maeneo ya hifadhi.
 
 

Saturday, September 24, 2016

Wafuasi wa Lipumba wakusanyika Buguruni kumwingiza ofisini

SeeBait

Vikundi vya wafuasi wa Profesa Ibrahim Lipumba wamekusanyika katika Ofisi za CUF Buguruni wakisubiri kumpokea mwenyekiti huyo wa zamani na kumwingiza ofisini.

Wanachama hao wanadai wana barua ya Msajili wa vyama vya siasa inayomtambua Profesa Lipumba kama mwenyekiti halali wa CUF.

Geti la ofisi za CUF limefungwa na ndani hakuna kiongozi yeyote wa chama.

Mashabiki hao wa Lipumba wanaoimba na kucheza, wanasema msafara wa Profesa uko njiani kuelekea kwenye ofisi hizo za makao makuu ya chama hicho.

Alipoulizwa kuhusu hali hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya CUF, Julius Mtatiro amesema ndio wamepokea barua ya msajili na bado wanaisoma ili kuona imeelekeza kitu gani.

Hata hivyo, Mtatiro amesema kwa vyovyote vile msajili wa vyama vya siasa hana mamlaka ya kuingilia maamuzi ya vikao vya chama chochote cha siasa.
 
 

Picha : Lowassa alipotembelea waathirika wa tetemeko la ardhi Bukoba

SeeBait
Aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, Edward Lowassa, leo amewasili Bukoba mkoani Kagera kuwatembelea na kuwajulia hali waathirika wa tetemeko la ardhi.

Tetemeko la ardhi lililotokea Bukoba mkoani Kagera Septemba 10 lilisababisha vifo vya watu 19 huku wengine zaidi ya 250 wakiachwa na maejeraha mbalimbali.

Alipofikika katika uwanja wa ndege wa Bukoba, Edward Lowassa aliyeambatana na  Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema , Sheikh Katimba, Khamis Mgeja na Mbunge wa Bukoba Mjini, Wilfred Lwakatare waliongozana hadi eneo la Hamugembe na Kashai kujionea madhara ya tetemeko la ardhi.

Akizungumza kwa nyakati tofauti na wananchi wa maeneo hayo, Lowassa aliwapa pole sana kwa yote yaliowafika na kusisitiza kwamba anaamini serikali itachukua jukumu la kuwasaidia.

Aidha, amesema kuwa msaada wake yeye atampatia Mkuu wa Mkoa, Meja Jenerali Mstaafu, Salum Kijuu ili uweze kuwasaidia wananchi wa Kagera.


Rais Magufuli Hajakataa Kuonana Na Viongozi Wa Dini:sheikh Alhad.

SeeBait

 Na.Sheila Samba & Abushehe Nondo,Maelezo
Viongozi wa Dini nchini, wamesema Rais JOHN MAGUFULI Hajakataa kuzungumza wala kuwapuuza viongozi hao ambao wamemuomba kukutana naye, kama inavyoenezwa na baadhi ya vyombo vya habari.

Akizungumza leo jijini, Dar es Salaam na waandishi wa habari Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhad Mussa Salum, amesema taarifa zilizochapishwa na gazeti la Tanzania Daima la Septemba 21 ISSN 0856 9762 toleo na.4310 sio za kweli.

“Taarifa hizo sio za kweli, taarifa hizo zimelenga kumgombanisha Rais na Viongozi wa Dini na watanzania kwa ujumla na hilo halitafanikiwa,” alisema Sheikh Alhad

Aidha Viongozi hao wamesema uamuzi wao wa kumuomba Rais kuonana naye, haujatokana na kuagizwa na UKAWA, bali umetokana na maono waliyopewa na Mwenyezi Mungu.

Amefafanua kuwa Rais MAGUFULI anawaheshimu Viongozi wa dini na mara zote amekua akiwaomba wamuombee na kusema leo ni siku ya tano tangu wamuandikie barua ya kumuomba kukutana naye na wanaimani Rais atakutana na Viongozi hao.

Ameeleza kuwa Barua hiyo imeandikwa Septemba 19 na kupelekwa siku hiyo hiyo Ikulu, ikiwa imesainiwa na Katibu Mkuu wa Bakwata, Katibu Mkuu wa CCT na Katibu Mkuu wa TEC.

“Naomba watanzania wasisikilize maneno hayo kwasababu hayana nia njema kwa Taifa letu, naamini Mh Rais tutaonana nae na tutaongelea mustakbali wa nchi katika mambo mbalimbali,” alisistisa Sheikh Alhad

 Akizungumzia utendaji wa Serikali ya Rais MAGUFULI, Sheikh ALHAD amesema Rais amerejesha nidhamu Serikalini, ukusanyaji mapato umeimarika na pia pengo kati ya wasionacho na walionacho linaanza kupungua.
 
 

Shirika La Ndege La Tanzania (Atcl) Lapewa Miezi 3 Kufumua Uongozi Uliopo.

SeeBait

WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa ametoa miezi mitatu kwa Bodi mpya ya Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) kusuka upya uongozi uliopo ili kuweza kuleta ufanisi wa utendaji kazi wa Shirika hilo.

Akizungumza jijini Dar es salaam mara baada ya kuitambulisha Bodi hiyo, Waziri Mbarawa amesema kuwa Uteuzi wa Bodi hiyo utasimamia kuleta tija na ufanisi wa shirika hilo ambalo kwa kipindi kirefu lilikuwa na changamoto nyingi.

“Nataka kuona mabadiliko makubwa kuanzia kwenye Menejimenti hadi uongozi wa chini, hakikisheni mnaweka uongozi amabao utafuata maadili, utakuwa na ufanisi, ubunifu na kasi katika utendaji kazi” amesema Profesa Mbarawa.

Aidha, ameitaka Bodi hiyo kusimamia na kuboresha mpango wa kibiashara wa usafirishaji (Business Plan) katika Shirika hilo ili kuweza kumudu soko la ushindani na kuweza kuongeza mapato ya Shirika hilo.

“Kama mnavyojua usafiri wa anga una ushindani mkubwa, hivyo ili Serikali iweze kupata faida katika biashara hii ni lazima tuboreshe mpango wa kibiashara unaoendana na wakati”, amesisistiza Waziri Mbarawa.

Profesa Mbarawa ameitaka Bodi hiyo kuipa ATCL mifumo imara, makini na mahiri ili kuweza kutatua changamoto zinazoikabili Shirika hilo ikwemo wizi wa mafuta ya ndege na upotevu wa mapato.

Ili kupima ufanisi wa utendaji wa Shirika hilo Profesa Mbarawa ameitaka Bodi hiyo kuandaa mkataba kwa kila mfanyakazi kuanzia ngazi ya juu hadi chini.

Katika hatua nyingine Waziri Mbarawa amesema kuwa Serikali ina mpango wa kununua ndege mbili mpya aina ya Jet ifikapo mwaka 2017 kwa lengo la kuboresha sekta ya usafirishaji wa anga nchini.

Kwa Upande wake, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani, ameitaka Bodi hiyo kutumia fursa walioipata katika kufanya kazi vizuri ili kufufua shirika hilo na kuwapatia watanzania huduma sahihi na bora za usafirishaji.

Naye, Mwenyekiti wa Bodi hiyo Mhandisi Emmanuel Korosso, ameahidi kushirikiana na wajumbe wa bodi yake katika kutekeleza maelekezo ya Waziri haraka iwezekanavyo ikiwemo kubadilisha menejimenti ya shirika hilo.

Imetolewa na Kitengo cha Habari na Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
 

Wenger ajibu mapigo baada ya Mourinho kudai alitaka kumharibu sura



1Arsene Wenger amekataa kujibu kauli ya hasimu wake Jose Mourinho kwamba siku moja angemharibu sura yake
Katika toleo la nne la kitabu cha ‘Jose Mourinho: Up Close and Personal’, Daily Mail imechapisha maneno ya Mourinho akisema alitaka kumharibu sura Arsene Wenger wakati akiwa meneja wa Chelsea msimu wa 2013-14
Akiongea kuelekea mchezo wa London derby dhidi ya Chelsea, Wenger amekataa kuzungumza chochote juu ya kauli hiyo ya Wenger.
“Sijasoma kitabu na hata hivyo sidhani kama nitakisoma,” aliwaamba wanahabari. “Sina cha kusema juu ya kauli hiyo.
“Mimi naongea kuhusu masuala ya soka tu. Mimi si mtu wa mrengo wa kuharibu mambo, nasema kamwe. Siku zote mimi ni mtu wa kujenga tu na siwezi kuongea chochote kuhusu hilo.
“Akili yangu yote inawaza kuhusu mchezo wa kesho na namna tutakavyoweza kucheza ili kupata matokeo.
“Sina matatizo binafsi na mtu yeyote yule. Namheshimu kila mtu katika tasnia yetu na sidhani kama ni vizuri sana kuzungumzia masuala ya timu nyingine.
“Uhasama binafsi ambao mnaousema haukuwa kwenye akili yangu. Kitu muhimu cha kuangalia ni kwamba tunaenda kucheza mchezo mkubwa wenye hisia kubwa.
Wenger anasherehekea maadhimisho ya miaka 20 ya muda wake aliotumikia Arsenal na endapo atashinda mchezo wa kesho dhidi ya Chelsea, basi furaha yake itakuwa mara mbili zaidi.
 

Match preview- Arsenal yenye njaa kuvunja mwiko wa muda mrefu dhidi ya Chelsea leo?



1Arsenal leo wako nyumbani wakiwa na mtihani mzito watakapokuwa wakiwakaribisha mahasimu wao wa jiji la London Chelsea katika mchezo wa EPL utakaofanyika kunako Uwanja wa Emirates saa 1:30 usiku kwa majira ya Afrika Mashariki.
Arsenal wanaingia katika mchezo huu wakiwa na imani kubwa kutokana na kuwa na kikosi imara msimu kunzia upande wa safu ya ulinzi mpaka ushambuliaji ukilinganisha na misimu kadhaa iliyopita.
Taarifa muhimu kwa kila timu
Mshambuliaji wa Arsenal Olivier Giroud leo anaweza kurejea baada ya kukosekana katika michezo miwli iliyopita kutokana na kusmbuliwa na majeraha.
Hata hivyo kiungo Aaron Ramsey bado ataendelea kuwa nje akiunguza jeraha lake la misuli ya paja na kukadiriwa kurudi takriban wiki tatu zijazo.
Kwa upande wa Chelsea, nahodha wao John Terry ataendelea kukosa mchezo wa leo ambao ni mchezo wa tatu mfululizo kufuatia kuendelea na tiba ya jeraha lake la mguu.
Beki mwenzake Mfaransa Kurt Zouma bado ataendelea kubaki nje licha kuwa tayari ameanza mazoezi madogo-madogo.
Kauli za makocha wa timu zote mbili
Kocha wa Arsenal Arsene Wenger juu ya nidhamu kwa timu yake: “Tumeongea kuhusu hilo kwasababu katika michezo miwili iliyopita dhidi ya Chelsea tumecheza tukiwa pungufu.”
“Hivyo mchezo wa leo utakuwa muhimu sana kwetu kupata matokeo, lakini muhimu zaidi kucheza kwa nidhamu kubwa.”
Kocha wa Chelsea Antonio Conte: “Huu ni mchezo mkubwa sana unawakutanisha mahasimu wakubwa. Ni muhimu zaidi kucheza soka safi.
“Zaidi ya hapo baada ya kufungwa na Liverpool kulitufedhehesha. Lakini leo itabidi tupambane sana maana tunafahamu kuwa tunacheza na si tu timu kubwa bali mahasimu wakubwa.”
Dondoo muhimu za mchezo
Head-to-head
  • Chelsea hawajapoteza mechi tisa zilizopita za Premier League dhidi ya Arsenal (wameshinda mara sita, droo mara 3).
  • Chelsea hawajapoteza mchezo wowote kati ya mitano ya mwisho waliyocheza katika Uwanja wa Emirates (ushindi mara 2, droo mara 3) tangu mara ya mwisho walivyofungwa 3-1 Desemba 2010. Na wameruhusu goli moja tu katika michezo yote hiyo.
  • Arsenal wameshinda kupata goli mbele ya Chelsea kwenye mechi sita zilizopita.
  • Katika mechi tano za mwisho dhidi ya Chelsea, jumla ya wachezaji wanne wa Arsenal wamejikuta wakitolewa nje kwa kadi nyekundu.
Arsenal
  • Arsenal wanajiandaa kupata ushindi wao wa nne mfululizo kwenye Premier League kwa mara ya kwanza tangu Oktoba mwaka 2015 walivyoweka rekodi ya kushinda mechi tano mfululizo.
  • Arsenal wamepoteza mchezo mmoja tu kati ya 15 iliyopita (wameshinda mara 8, droo mara nne).
  • Alexis Sanchez ameshindwa kufunga hata goli moja kwenye michezo minne ya ligi akiwa kwenye Uwanja wa Emirates.
Chelsea
  • Kocha wa Chelsea Antonio Conte anaweza kucheza michezo mitatu bila ya ushindi kwa mara ya kwanza tangu mara ya mwisho walivyopata sare nne mfululizo wakati akiwa Juventus Macih 2012.
  • Conte hajawahi kupoteza michezo ya ligi mfululizo tangu Desemba 2009 wakati akiwa Atlanta.
  • Chelsea wamepata clean sheet moja tu kwenye michezo yao ya ligi 12 iliyopita, huku wakiruhusu bao kwenye kila mchezo kati ya michezo sita iliyopita ya ugenini.
  • Diego Costa amefunga magoli matano kwenye michezo mitano ya Premier League msimu huu, akifunga kwenye kila mchezo kati ya mitatu iliyopita.


KIPRE TCHETCHE AREJEA OMAN KUPIGANIA UHAMISHO WAKE AZAM FC


MSHAMBULIAJI Kipre Herman Tchetche amerejea Oman kupigania uhamisho wa kuanza kuichezea klabu yake mpya, Al-Nahda Al-Buraimi kutoka Azam FC ya Tanzania. Tchetche alilazimika kurejea kwao, Ivory Coast mapema mwezi huu baada ya Azam FC kugoma kumruhusu kujiunga na Al Nahda bila dola za Kimarekani 50,000. Na Azam ilifanya hivyo kwa sababu Tchetche aliondoka Dar es Salaam akiwa amebakiza Mkataba wa mwaka mmoja baada ya kuichezea klabu hiyo tangu mwaka 2010.  
Kipre Tchetche amerejea Oman kupigania uhamisho wake kutoka Azam FC 
Hata hivyo, akizungumza na BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE leo kutoka Muscat, Oman, Tchetche amesema anatarajia kumalizana na Azam FC ndani ya muda mfupi tangu sasa. “Tayari nimerudi Oman na ninatarajia kumalizana na Azam muda si mrefu ili nianze kucheza hapa,”alisema.     Kipre Tchetche alijiunga na Azam FC mwaka 2011 kwa pamoja na pacha wake, Kipre Michael Balou baada ya wote kung’ara katika kikosi cha Ivory Coast kilichokuja kucheza michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati (CECAFA Challenge) Dar es Salaam. 
 
 

WACHEZAJI KILIMANJARO QUEENS KUPEWA AJIRA...ZAWADI YA UBINGWA CHALLENGE


UBINGWA wa Kombe la CECAFA Chalenji kwa timu za mpira wa miguu za wanawake katika nchi za Afrika Mashariki, umewavutia wadau wengi kwa kiwango kikubwa hivyo kushusha neema kwa wachezaji hao wa timu ya taifa ya Tanzania Bara maarufu kama Kilimanjaro Queens ambayo imeandika historia ya kutwaa taji hilo ikiwa ni taifa la kwanza katika mashindano hayo mapya. Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye, amefurahishwa na ubingwa wa timu hiyo akisema: “Si ubingwa tu, bali umefuta dhana ya Wakenya ambao siku zote wamekuwa wakitangaza Mlima Kilimanjaro uko kwao Kenya wakati upo hapa Tanzania. Kwa kuifunga Kenya, mmefanya kazi nzuri.”.
Kutokana na ubingwa huo na kuitetea nchi, Nape ambaye aliongozana na Wabunge sita wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliahidi kuitafutia timu hiyo ya taifa ya wanawake mdhamini na kwa baadhi ya wachezaji kupata ajira sehemu mbalimbali hususani kwa makampuni kadhaa ambayo yamewekeza hapa nchini. “Niko na Wabunge hapa. Bunge la Novemba ambalo litaanza Novemba mosi, naawaalika bungeni. Tutazungumza na Spika ili kuvunja kanuni za bunge ilo ninyi muingie bungeni la kombe letu. Nitawaomba wabunge wakate posho zao kidogo, ili kuwazawadia ninyi pale mtakapofika. Tutakuwa na mchezo wa mpira wa miguu kati yenu na wabunge, na kila bao moja mtakalowafunga wabunge, litalipiwa Sh milioni moja.” “Mimi ndiye nitakayehesabu mabao, lakini mkae mkijua haitakuwa kazi rahisi kuwafunga wabunge. Wako vizuri,” alisema Nape ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Mtama na kauli yake hiyo iliungwa mkono na Mwenyekiti wa Bunge Sports Club, William Ngeleja aliyeambatana wabunge wengine akiwamo Makamu Mwenyekiti wa Bunge Sports Club, Esther Matiko. Wengine waliokuwako ni Bupe Mwakang’ata, Alex Gashaza, John Kanuti ambaye mbali ya ubunge pia ni Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF kadhalika Venance Mwamoto – nyota wa zamani wa timu ya Taifa na Kocha wa daraja B. Kwa upande wa TFF, Rais wa Shirikisho la Miguu Tanzania, Jamal Malinzi alitoa ahadi ya Dola za Marekani 10,000 (sawa na Sh milioni 22) kwa timu hiyo baada ya kutwa taji hilo kabla ya timu hiyo leo kutembelea Kampuni ya Airtel ambako Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Airtel-Tanzania, Beatrice Singano akatangaza kampuni yake kuendelea kudhamnini mashindano ya kuibuka vipaji ambavyo vimekuwa vikiitoa Tanzania kimasomaso katika mashindano ya kimataifa. Kati ya nyota 20 wa Kilimanjaro Queens waliotwaa taji hilo, wanane walipitia mashindano ya Airtel kwa miaka tofauti katika udhamini ambao kwa mwaka huu ilikuwa ni mara ya sita kwa kampuni hiyo inayofanya vema kwenye soko la huduma za simu, kudhamini mashindano ya Airtel Rising Stars (ARS). Safari ya ubingwa wa Kilimanjaro Queens ulianzia hatua ya makundi kwa kuilaza Rwanda manbao 3-2 kabla ya kutoka sare tasa na Ethiopia ambayo pia ilivuna ushindi wa mabao 3-2 kutoka kwa Rwanda. Tanzania na Ethiopia zilitoka sare na kurusha sarafu ambako Tanzania ikawa ya kwanza katika kundi B hivyo kucheza na Uganda ambayo ililala kwa mabao 4-0 katika mchezo wa nusu fainali. Na Septemba 20, 2016 ikatawazwa kuwa mabingwa kwa ushindi wa mabao 2-1. Timu zote shiriki zilikuwa Tanzania, Burundi, Zanzibar, Kenya, Ethiopia, Rwanda pamoja na mwenyeji Uganda. Mashindano ya Kombe la Chalenji la CECAFA kwa timu za wanawake yamefanyika kwa mara ya kwanza jambo linaloleta tafsiri kuwa michuano hiyo inaweza kuinua soka la wanawake kwa ukanda wa nchi za Afrika Mashariki na Kati.

RIPOTI SPESHO

MOURINHO AKANUSHA NUKUU YA ‘KUBOMOA SURA YA WENGER’!


WENGER-MOURINHOJose Mourinho amesema hana tatizo na Arsene Wenger licha ya kuchapishwa Kitabu kikimnukuu yeye akisema ‘ataibomoa Sura ya Wenger’.
Mourinho, ambae sasa ni Meneja wa Manchester United, amekuwa na upinzani wa muda mrefu na Wenger ambae ni Meneja wa Arsenal na hasa wakati Mourinho akiwa ni Meneja wa Chelsea.
Akiwa huko Chelsea, Mourinho aliwahi kumbatiza Wenger kuwa ni ‘Spesho wa Kushindwa’.
Nukuu hiyo ya kwamba ‘ataibomoa Sura ya Wenger’ ipo kwenye Kitabu kiitwacho Jose Mourinho: Up Close and Personal  kilichaoandikwa na Mwanahabari Rob Beasley.
Jana, Wenger alipogusiwa kuhusu Kitabu hicho alisema hatakisoma.
Na Jana hiyo hiyo, Mourinho akaulizwa kuhusu Kitabu hicho na kujibu: “Utaona yuko karibu na mimi. Nina furaha. Ametengeneza Pesa zake, hilo sawa kwangu!”
Mourinho aliongeza: "Nilikutana na Arsene Wenger Wiki chache zilizopita, na kama Watu wastaarabu, tukapeana mikono. Tukakaa Meza moja na kula Chakula cha Usiku pamoja na Watu wengine. Tukabadilishana mawazo, tuliongea kwa sababu sisi ni Watu tuliostaarabika. Kwa mara nyingine sidhani Kitabu hiki kitakaa Maktaba moja na vile vya Shakespeares na vingine!”
Aliongeza: “Sitaongeza lolote jingine. Hilo ni neon langu la mwisho. Narudia huyo ametengeneza Pesa yake. Hilo sawa kwangu!”

kimataifaaa
 
Mahakama ya Kikatiba ya Gabon imemthibitisha Rais Ali Bongo Ondima kuwa mshindi wa uchaguzi wa mwezi uliopita. Kumekuwa na wasiwasi kuwa tangazo hilo lililotolewa mapema leo linaweza kuzusha vurugu zaidi, katika taifa hilo lenye utajiri wa mafuta, ambalo familia ya Bongo imekuwa madarakani kwa nusu karne sasa. Mvutano umekuwa mkali tangu yaliopotolewa matokeo ya awali yalikuwa yakionesha Rais Bongo amemshinda mgombea wa upinzani, Jean Ping, kwa kiwango kisichozidi asilimia mbili za kura. Ping vile vile alidai ameshinda uchaguzi wa Agosti 27, na alikwenda mahakamani kutaka kuhesabiwa upya kwa kura. Upinzani unasema takribani watu 100 wamekufa katika vurugu za baada ya uchaguzi, wakati serikali ikisema ni watu watatu tu, ndio waliokufa katika vurugu hizo. Zaidi ya watu 1,200 wamewekwa kizuizini. Bongo aliingia madarakani 2009 baada ya kifo cha baba yake, Omar Bongo, aliyeongoza kwa miaka 42 kufariki.
Watu 93 wameuwawa jimboni Aleppo, kaskazini mwa Syria, ikiwa ikiwa takribini siku ya pili mashambulizi makali. Taarifa hiyo ni kwa mujibu wa kundi moja la uokozi liitwalo White Helmets. Wakaazi katika eneo linalodhibitwa na waasi wanasema majengo ya vituo vya dharura yameshambuliwa na makaazi kuharibiwa vibaya. Ibrahim al Hajji anaefanya kazi ya kujitolea katika kundi hilo anasema wakaazi katika mji huo uliozingirwa hawawezi kutoka na watu kwa kiasi kikubwa wamekuwa na wasiwasi majumbani mwao. Umoja wa Mataifa unakadiria kiasi cha watu 250,000 wamenasa kwenye eneo hilo linaloshikiliwa na waasi.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Frank-Walter Steinmeier, amesema wapiga kura wa Marekani watachagua kujihusisha au kujiondoa katika jumuiya ya kimataifa katika uchaguzi ujao wa rais. Akihutubia Baraza Kuu ya Umoja wa Mataifa, Steinmeier alielezea kile alichokiita machaguo yanaoukabili ulimwengu kuwa ni kukabiliana na ugaidi, mabadiliko ya tabia nchi na janga la uhamiaji. Waziri huyo pasipo kutaja majina ya mgombea  Donald Trump wa chama cha Republican au Hillary Clinton wa Democrat, alisema nayo Marekani inayokabiliwa na uchaguzi katika kipindi cha wiki sita zijazo, itaamua ama kuunga mkono kujiondoa katika shida zinazougumbuka ulimwengu, ambazo baadhi wanatoa wito wa ushirikiano wa kimataifa kutataka kuzitatua. Steinmeir ametumia hotuba yake hiyo mbele ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kutoa wito wa kurejeshwa hali ya kusitisha mapiganio Syria, na kutoa wito kwa serikali ya Syria inayoongozwa na Bashar al-Assad kusitisha mashambulizi ya angani na kuruhusu misaada ya kiutu.

Familia ya mtu aliyeuwawa kwa kupigwa risasi huko North Carolina, Marekani, imetoa vidio inayoonesha kifo chake. Mvutano umezidi kuongezeka wakati polisi kwa upande wao inakaidi kuonesha vidio yake ya tukio hilo. Siku ya tatu ya maandamano dhidi ya hatua za polisi kuwafyatulia risasi hasa Wamarekani Weusi, ilikuwa tulivu baada ya siku mbili za vurugu, zilizosababisha mtu mmoja auwawe kwa kupigwa risasi na raia, watu tisa kujeruhiwa na wengine 44 kukamatwa Jumatano na Alhamis asubuhi. Vile vile, kulikuwa na uporaji na uharibufu mkubwa, mambo ambayo yalisababisha meya kutangaza amri ya kutotoka nje nyakati za usiku. Wakati huo huo, mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya Democrat, Bi Hillary Clinton, ameahirisha ziara yake katika mji wa Charlotte, yalikotokea mauaji hayo. Taarifa ya timu yake ya kampeni inasema, licha ya kupokea mualiko wa kwenda huko kutoka kwa viongozi wa kijamii, wamekubaliana sasa kuifuta safari hiyo.

Watu 13 wameuwawa kufuatia mapigano kati ya polisi na wanamgambo wanaolipiza kisasi cha kuuawa kwa kiongozi wao, katikati mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Vyombo vya habari vya nchini humo pamoja na mashahidi wanasema mapigano hayo yaliyodumu kwa siku mbili katika mji wa Kananga, ambapo wapiganaji watiifu kwa kiongozi wa kimilia, Chifu Kamwina Nsapu, aliyeuawa katika makabiliano na polisi mwezi uliopita, waliingia kwa mara ya kwanza asubuhi ya Alhamis. Kwa mujibu wa Redio Okapi, wapiganaji wanane wameuwawa na vikosi vya usalama kabla hawajatoroka na kisha kurudi tena, huku watoto wa shule watatu na mtu mmoja nao wakiuawa. Hayo yanatokea ikiwa siku chache baada ya kutokea vurugu nyingine katika mji mkuu Kinshasa, ambapo upinzani ulisema takribani waandamanji 100 wanaopinga Rais Joseph Kabila kujiongezea muda madarakani waliuawa.



 
 
habari za jumamosi ya leooo habari za jumamosi ya leooo Reviewed by RICH VOICE on Septemba 24, 2016 Rating: 5

Hakuna maoni

Chapisho Lililoangaziwa

Thursday, September 15, 2016 Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Alhamisi Ya Septemba 15 ...