Wahusika wakuu mzozo wa kisiasa Zimbabwe

Mugabe na mkewe wamezozana na aliyekuwa makamu wake Emmerson Mnangagwa (pili kulia) na mkuu wa majeshi Jenerali Constantino Chiwenga

Haki miliki ya pichaAFP/REUTERS/EPA
Image captionMugabe na mkewe wamezozana na aliyekuwa makamu wake Emmerson Mnangagwa (pili kulia) na mkuu wa majeshi Jenerali Constantino Chiwenga
Wakuu wa jeshi nchini Zimbabwe wamesema wanachukua udhibiti wa serikali kuondoa "wahalifu" wanaomzingira Rais Robert Mugabe na kusababisha mzozo wa kisiasa nchini humo.
Hayo yamejiri wiki moja baada ya Mugabe kumfuta kazi makamu wake Emmerson Mnangagwa, hatua iliyoonekana kuchochewa na mkewe wake Grace, ambaye amekuwa akitaka kuwa makamu wa rais.
Mkuu wa majeshi Jen Constantino Chiwenga alitoa onyo Jumatatu kwamba jeshi halitasita kuchukua hatua iwapo hatua za kuwaondoa wapinzani katika chama tawala cha Zanu-PF hazitakomeshwa.
Nani wahusika wakuu mzozo wa sasa wa kisiasa?

Robert Mugabe

Zimbabwean President Robert Mugabe addresses a meeting of his ruling Zanu-PF party's youth league in Harare, Zimbabwe, on 7 October 2017Haki miliki ya pichaREUTERS
Robert Mugabe alikuwa shuja mwanamageuzi aliyekaa jela kwa miaka mingi akipigania uhuru wa Zimbabwe. Aliingia madarakani baada ya uchaguzi kufuatia uhuru wa Zimbabwe mwaka 1980.
Ndio maana, hadi wa leo, wengi wa viongozi wa Afrika huchelea kumkosoa - kinyume na raia wengi nchini mwake ambao wamekumbana na utawala wake.
Mataifa mengi duniani yamesonga mbele kutoka kwa vita dhidi ya wakoloni, lakini mtazamo wa Mugabe na juhudi zake za kudumisha udhibiti wa kisiasa zimesalia kuwa zile zile.
Anafahamika sana kwa mpango yake ya mageuzi ya umiliki wa ardhi miaka ya 1990, ambapo mashamba yaliyomilikiwa na Wazungu yalitwaliwa na kupewa wakulima Waafrika.
Baada ya miongo ya utawala wake wa kiimla, taifa lake limo kwenye mzozo wa kisiasa na kiuchumi.
Tuhuma za ufisadi serikalini zimesheheni.
Mugabe, 93, amekuwa hataki kuachia mamlaka lakini kimwili amedhoofika kutokana na umri.
Mjadala kuhusu mrithi wake umekuwa ukitawala siasa humo.
Wanasiasa wa kizazi cha wazee waliopigania uhuru wakiwakilishwa na Mnangagwa wamekuwa wakishindana na kizazi cha wanasiasa wa umri mdogo maarufu kama "Generation-40" wanaoungwa mkono na Bi Mugabe.

Grace Mugabe

Zimbabwean President Robert Mugabe's wife Grace Mugabe looks on during a national church interface rally in Harare, Zimbabwe, on 5 November 2017Haki miliki ya pichaREUTERS
Grace Mugabe, mke wa pili wa Robert ni mdogo wake kwa umri kwa miaka 40.
Alikuwa karani wa rais huyo lakini alipanda ngazi na kuwa mwanamke mwenye nguvu zaidi Zimbabwe.
Walikutana na kujaliwa watoto wao wawili kati ya watatu mke wa kwanza wa Mugabe, Sally, alipokuwa anaugua saratani.
Hata hivyo, walifunga ndoa rasmi baada ya kifo chake.
Anadaiwa kuwa na kiu sana ya maisha ya kifahari na vitu vya thamani, kiasi kwamba amebandikwa jina Gucci Grace.
Wafuasi wake hata hivyo humsifu sana kwa juhudi zake za kusaidia wasiojiweza na humuita "Dr Amai", kwa maana ya "mama".
Lakini wakosoaji wake wanasema amekuwa akiendesha juhudi za kujitajirisha na kujilimbikizia mamlaka.
Kama mmoja wa watu walio karibu sana na rais, Grace amewekewa vikwazo na EU na Marekani sawa na mumewe. Vikwazo hivyo ni pamoja na mrufuku ya usafiri na kuzuiliwa kwa mali.
Huwa anaandamana na rais safari zake ng'ambo, sawa Mashariki ya Mbali ambapo wanamiliki mali.
Miongoni mwa biashara nyingine zake nyumbani ni shamba la ng'ombe wa maziwa viungani mwa Harare, ambalo alijitwalia kama sehemu ya mageuzi kuhusu umiliki wa ardhi yaliyoanza kutekelezwa 2001.
Bi Mugabe huwa mkali sana kwa maneno na wiki iliyopita alimweleza mpinzani wake, makamu wa rais Mnangagwa, kama "nyoka" ambaye "lazima agongwe kichwani". Siku iliyofuata, Rais Mugabe alimfuta kazi Mnangagwa.

Emmerson Mnangagwa

Emmerson Mnangagwa on 1 November 2017, before he was sacked as vice-presidentHaki miliki ya pichaEPA
Hadi ushawishi wa Bi Mugabe ulipozidi, Emmerson Mnangagwa alikuwa akitazamwa na wengi kama mrithi mtarajiwa wa Rais Mugabe.
Baada ya kupokea mafunzo ya kijeshi Misri na China, alisaidia kuelekeza vita vya ukombozi kabla ya uhuru 1980.
Alifungwa jela na inadaiwa kwamba aliteswa.
Amekuwa kwenye serikali tangu uhuru.
Maelfu ya raia walifariki katika vita vya baada ya uhuru ambavyo alichangia kama waziri wa usalama wa taifa, ingawa anasema hafai kulaumiwa.
Hufahamika sana Zimbabwe kama "ngwena" au "mamba" (na wafuasi wake hufahamika kama "Lacoste") kwa sababu ya ujanja wake katika siasa.
Alijipanga upya miaka ya 1990 na kurejea kuwa na ushawishi serikali baada ya kuzozana na Bw Mugabe na kutupwa nje.
Lakini umaarufu wake una maana kwamba hapendwi sana na wengi wanaomuunga mkono Mugabe katika chama cha Zanu-PF.
Kama waziri wa zamani wa ulinzi na usalama wa taifa miongoni mwa nyadhifa nyingine, alikuwa kiungo muhimu katika uhusiano wa chama tawala na jeshi la Zimbabwe na mashirika ya kijasusi.
Amekuwa pia ni mwenyekiti wa Kundi la Pamoja na Shughuli za Kiusalama, ambalo husimamia usalama wa taifa.

Jen Constantino Chiwenga
Gen Constantino Chiwenga, chief of Zimbabwe's armed Forces, on MondayHaki miliki ya pichaAFP
Jenerali Constantino Chiwenga, 61, ni mshirika wa karibu wa Bw Mnangagwa, na ameongoza majeshi ya Zimbabwe tangu 1994.
Jen Chiwenga alikuwa kwenye vita vya uhuru, na alipokea mafunzo akiwa na Jeshi la Ukombozi wa Zimbabwe nchini Msumbiji na kisha akapanda cheo.
Mwaka 2002, Chiwenga na washirika wengine 18 wa karibu wa Bw Mugabe waliwekewa vikwazo na Umoja wa Ulaya, Marekani na New Zealand, ikiwa ni pamoja na marufuku ya usafiri na kuzuiliwa kwa mali yao.
Vikwazo hivyo vimekuwa vikiongezwa muda wake. Mwaka 2003, alipandishwa cheo na kufanywa kamanda jenerali wa Majeshi ya Ulinzi ya Zimbabwe.
Aliwashangaza raia wengi wa Zimbabwe Jumatatu alipotoa onyo hadharani kwa wale waliokuwa wanawatimua wengine - waliohusika vita vya ukombozi dhidi ya wakoloni - katika chama tawala cha Zanu-PF akisema jeshi lingeingilia kati.
Wahusika wakuu mzozo wa kisiasa Zimbabwe Wahusika wakuu mzozo wa kisiasa Zimbabwe Reviewed by RICH VOICE on Novemba 15, 2017 Rating: 5

Hakuna maoni

Chapisho Lililoangaziwa

Thursday, September 15, 2016 Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Alhamisi Ya Septemba 15 ...